23.6 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Maonesho ya biashara Mwanza yaanza, TCCIA yalia mitaji kuyumba

Na Clara Matimo, Mwanza

 Maonesho ya 16 ya  biashara Afrika Mashariki yanayoandaliwa na  Chemba ya Wafanyabiashara, Wenye Viwanda na Kilimo  Tanzania (TCCIA) Mkoa wa Mwanza yameanza leo katika viwanja vya Rock City Mall jijini hapa yakikusanya wafanyabiashara zaidi ya 190 kutoka nchi za Indonesia, India, Nigeria na wenyeji Tanzania.

Akizungumzia maonesho hayo, Mwenyekiti wa TCCIA Mkoa wa Mwanza, Gabriel Kenene amesema, ufunguzi rasmi utafanyika Agosti 31 na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhandisi Robert Gabriel, yatahitimishwa Septemba tano mwaka huu.

Amesema maonyesho ya mwaka huu yamepungua nguvu kutokana na baadhi ya nchi za Afrika Mashariki  ikiwemo Uganda, Kenya, Burundi  na Rwanda kutoshiriki kufuatia madhara ya janga la UVIKO 19 ambayo yamesababisha mitaji ya kampuni nyingi kuyumba.

Kwa mujibu wa Kenene, walitarajia kupata kampuni  310 lakini hadi sasa  yaliyothibitisha kushiriki ni kampuni 190 ambapo mwaka jana yaliyoshiriki ni 185 kati ya 250 yaliyotarajiwa kuwepo huku sababu za UVIKO 19 zikitajwa kutokana na baadhi ya nchi za Afrika Mashariki kutofungua mipaka yake.

“Mwaka kesho tunatarajia kushirikisha zaidi ya kampuni 600 tunataka tuanze maandalizi mapema baada ya haya kukamilika, tutaanza kuandaa yanayokuja mara tu haya yatakapokamilika, tunaamini hata ugonjwa wa korona utakuwa umepungua pia matarajio yetu ni kuwashirikisha hadi mama na baba lishe,”amesema.

Kenene ametaja faida za maonyesho hayo kuwa ni pamoja na kuinua uchumi wa ndani ya nchi pia Serikali inapata mapato yatokanayo na ushuru unaolipwa huku  wafanyabiashara wa ndani wakipata fursa ya kujifunza kutoka kwa wageni na kuongeza ubunifu.

Baadhi ya washiriki wa maonyesho hayo akiwamo Atwia Haruna na Yusuph Mohammedi wameishauri TCCIA kuondoa gharama za kiingilio  kwa wananchi ili wengi waweze kuingia uwanjani hapo na kununua bidhaa mbalimbali watakazozipenda.

Wamesema faida watakazozipata ni pamoja na kuongeza mtandao wa mahusiano, kupata fursa za masoko na kukuza biashara zao kwa kuongeza wateja.

Haruna ambaye ni Mkurugenzi wa Kampuni ya Egyptian wauzaji wa vyakula  vya asili, amesema maonesho hayo yamemuongezea ubunifu katika kutengeneza  bidhaa zake ambapo amebainisha kwamba lengo lake ni kuwa mshiriki wa kudumu ili azidi kuongeza wateja na hatimaye awe mfanyabiashara mkubwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles