27.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

MALENGO YA MAPINDUZI SI KUBAGUANA – DK. SHEIN


Na Mwandishi Wetu – Chake Chake

RAIS wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein, amesema kuwa malengo ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964 ni kuzifanya hali za maisha ya Wazanzibari kuwa bora na si kubaguana kwa vyama, dini, jinsia au mahala mtu anapotoka.

Dk. Shein aliyasema hayo jana mara baada ya kuzindua soko jipya la Tibirinzi, Chake Chake Pemba ikiwa ni miongoni mwa shamrashamra za kutimiza miaka 54 ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Januari 12, 1964.

Alisema kuwa soko hilo si vyema likahusishwa na masuala ya kisiasa kwani ni la watu wote, wa vyama vyote, dini zote na jinsia zote, huku akiwataka wafanyabiashara watakaolitumia kuleta bidhaa zenye ubora zitakazolingana na hadhi yake.

Dk. Shein amesisitiza kuwa jengo hilo jipya la soko ni ukombozi kwa wakulima, wafanyabiashara, wafugaji, wavuvi, wajasiriamali na wananchi wote kwa jumla kwa kuweza kuongeza kipato chao ili maisha yao yaweze kuwa bora.

Alisema kuwa ujenzi wa soko hilo ni katika hatua za kutafsiri Mapinduzi ya mwaka 1964 kwa vitendo kwa kuwaletea wananchi maendeleo zaidi bila ya ubaguzi.

Alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inatekeleza sera mbalimbali zikiwamo zinazolenga kuinua kipato cha wananchi na kupunguza umasikini.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alisisitiza haja ya kulitunza na kulienzi soko hilo ikiwa ni pamoja na kudumisha usafi aliosema ni jambo la lazima na halina mbadala.

Alieleza madhumuni makubwa ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kuwa huru, hatua ambayo imewezesha kupanga mambo bila ya kuingiliwa na mtu na kuweza kuongoza nchi sambamba na kuandaa mipango ya muda mrefu, mfupi na wa kati.

Alisema kuwa Zanzibar imepata maendeleo makubwa katika kukuza uchumi wake ndani ya kipindi cha miaka 54, kukiwa na mabadiliko makubwa ya kiuchumi.

Naye Waziri wa Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi, Hamad Rashid Mohammed, alieleza kuwa kuna kila sababu ya kumuenzi na kumwombea dua Dk. kwa juhudi anazozichukua katika kuwaletea maendeleo wananchi wa Zanzibar.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles