23.2 C
Dar es Salaam
Saturday, July 27, 2024

Contact us: [email protected]

Magonjwa yawaandama nyota wa Yanga

Pluijm1NA ADAM MKWEPU, DAR ES SALAAM

WACHEZAJI nyota wa Yanga wanaandamwa na magonjwa mbalimbali yanayoweza kukiathiri kikosi hicho katika mchezo wao wa mzunguko wa pili wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Coastal Union, utakaofanyika Jumamosi hii.

Wachezaji wenye matatizo ndani ya kikosi hicho ni Amissi Tambwe, ambaye ana maumivu ya sikio, Issoufou Boubacar anayesumbuliwa na tumbo na kipa Deogratius Munishi, anayesumbuliwa na malaria.

Kutokana na hali hiyo, Kocha Mkuu wa Yanga, Hans van der Pluijm, aliliambia MTANZANIA jana kuwa hana wasiwasi wa kupata ushindi, kwani wamepania kuendeleza kasi yao Ligi Kuu na kuhakikisha wanaendelea kubaki kileleni.

Alisema wachezaji hao walipata matatizo baada mchezo uliopita wa Kombe la FA dhidi ya Friends Rangers uliofanyika katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam ambapo Yanga ilishinda mabao 3-0.

Kocha huyo raia wa Uholanzi alisema kuwa, pamoja na kikosi hicho kuwa na majeruhi wengi, bado ana matumaini makubwa ya ushindi kwa kuwa wachezaji wote 24 waliowasajili msimu huu wana viwango vya kimataifa.

“Yanga ni timu kubwa iliyosajili wachezaji wazawa na wa kimataifa wenye sifa na viwango vinavyokubalika, hivyo siwezi kupata wasiwasi wa kupata ushindi kutokana na kuwepo kwa majeruhi wengi,” alisema.

Alisema beki Nadir Haroub ‘Cannavaro’ ambaye ni majeruhi wa muda mrefu, tayari ameondolewa bandeji ngumu aliyokuwa amefungwa, jambo linaloashirikia kuwa anaendelea vizuri.

 

Akizungumzia kiwango cha kiungo wa kimataifa wa Rwanda, Haruna Niyonzima, aliyekosa mechi nyingi za Ligi Kuu kutokana na kusimamishwa na uongozi wa klabu hiyo, Pluijm alisema bado anahitaji muda zaidi wa kujiweka fiti, ili aweze karudi katika ubora wake.

Mabingwa hao watetezi wanaoongoza katika msimamo wa ligi kwa kujikusanyia pointi 39, wanatarajia kuanza duru ya mzunguko wa pili kwa kucheza ugenini dhidi ya wenyeji Coastal katika Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.

Katika mzunguko wa kwanza Yanga walibanwa mbavu katika uwanja huo na kupata suluhu walipokutana na Mgambo Shooting, kabla ya kuibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya African Sports.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles