24.7 C
Dar es Salaam
Tuesday, March 19, 2024

Contact us: [email protected]

Magonjwa yasiyoambukiza yanavyogharimu taifa

Na AVELINE KITOMARY

KWA mujibu wa wataalamu magonjwa yasiyoambukiza ni aina ya magonjwa yasiyo na vimelea vinavyoweza kusambazwa kutoka kwa mtu mmoja hadi mwingine.

Miongoni mwa magonjwa hayo ni saratani, kisukari, magonjwa ya moyo, mishipa ya damu, selimundu, magonjwa ya akili, magonjwa sugu ya njia ya hewa, magonjwa ya figo, dawa za kulevya, ajali na magonjwa ya meno na macho.

Jambo la kushtua ni kuwa magonjwa haya yanaongezeka kwa kasi na kuwaathiri hata watu wenye umri mdogo ambapo kwa miaka nane sasa watoto na makundi ya vijana wamekuwa waathirika.

Hata hivyo wataalamu wameainisha sababu mbalimbali ya kuongezeka kwa ugonjwa huo ikiwemo mtindo mbaya wa maisha na kutokufanya mazoezi.

Takwimu zilizotolewa na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsi, Wazee na Watoto zinaeleza kuwa magonjwa yasiyoambukiza(Non-Communicable Diseases) yanaendelea kuongezeka nchini ambapo jumla ya vifo 134,600 viliripotiwa sawa na asilimia 33 mwaka 2017.

Takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) zinaonesha kuwa magonjwa yasiyoambukiza yanachangia zaidi ya vifo milioni 41 ambayo ni sawa na asilimia 71 ya vifo vyote milioni 57 vilivyotokea mwaka 2016.

Vifo vinavyotokea nchini vinatokana zaidi na magonjwa ya moyo na shikizo la damu kwa asilimia 13, kisukari asilimia mbili, saratani asilimia saba na ajali asilimia 11tu.

YANAVYOGHARIMU TAIFA

Akizungumza katika uzinduzi wa kongamano la pili la kisayansi lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) Mganga Mkuu wa Serikali, Prof. Abel Makubi anasema magonjwa yasiyoambukiza yanaigharimu sana Taifa.

“Magonjwa haya yanasababisha hasara kubwa kwa Taifa kwa maana ya kuondoa nguvu kazi na kurudisha nyuma maendeleo ya mtu binafsi na taifa kwa ujumla.

“Hali hiyo husababisha utegemezi sugu kwa familia na Pia kuongeza mzigo mkubwa kwenye mfumo wa afya kwa kuwa ni magonjwa ya muda mrefu na yanatumia rasilimali,”anabainisha Prof. Makubi.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Huduma za matibabu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Dk. David Mwenesano anasema kwa magonjwa yasiyoambukiza gharama za matibabu ni kubwa hivyo serikali hutumia gharama nyingi kutibu wananchi wake.

“Mgonjwa yasiyoambukiza yapo katika bima ya afya kama saratani tunalipia matibabu na uchunguzi,magonjwa ya moyo, figo, tunaangalia gharama ni jinsi gani tunashusha kwani gharama ni

kubwa na tunatumia fedha nyingi mfano dozi moja ya saratani ni Sh. milioni 4.7 hivyo serikali inatumia fedha nyingi ukizingatia wagonjwa wengi hawana uwezo wa kumudu matibabu hayo,” anasema Dk. Mwenesano.

Akihitimisha wiki ya magonjwa yasiyoambukiza, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Abobakar Kunenge anasema kuwa inabashiriwa kuwa ifikapo mwaka 2033 gharama zitokanazo na huduma ya magonjwa hayo yatafikia dola za Marekani trilioni47.

Anasema kiasi hicho cha fedha zingeweza kupunguza umasikini kwa watu bilioni 2.5 kwa miaka 50 na kwa nchi za uchumi wa kati na chini magonjwa hayo yanagharimu dola trilioni saba kwenye kipindi cha 2011-2025.

“Gharama hizo zinatokana na huduma za matibabu na nguvu kazi inayopotea na makadirio yanaonesha kuwa gharama za huduma kwa wagonjwa yasiyoambukiza itafikia asilimia 75 ya mzigo wote wa bajeti ya Afya duniani huku ugonjwa wa kisukari

pekee ukipelekea gharama zaidi ya dola za bilioni 465 sawa na asilimia 11 ya bajeti yote ya Afya duniani,”anabainisha Kunenge.

Akitoa mifano ya gharama za huduma za afya nchi Kungene anasema wagonjwa wa matatizo ya figo kushindwa kufanya kazi wanahitaki huduma ya kusafisha damu angalau mara tatu kwa wiki moja ambapo matibabu hayo yanachukua gharama kubwa.

“Gharama za kusafisha kwa kiwango cha kawaida katika hospitali za serikali ni Sh 200,000 kwa siku bila ya gharama nyingine ya matibabu, usafiri na chakula kwa wiki mmoja mgonjwa atatumia Sh 600,000 na kwa mwezi Sh milioni 2.4 ambayo ni sawa na Sh milioni 28 kila mwaka.

“Gharama hii ni kubwa kwa

watanzania wengi lakini gharama za kuzuia tusipate madhara yatokanayo na magonjwa haya ni nafuu sana hivyo tunawaasa wananchi kuzingatia msemo wa Kinga ni Bora, Kuliko Tiba kwa sababu tatizo hilo lipo nchini na linaongezeka kwa kasi, kuna ongezeko la asilimia 24 ndani ya miaka miwili ni kubwa linahitaji mikakati kukabiliana nalo,”, anafafanua.

JE DAWA ASILI ZITASAIDIA?

Zipo dhana mbalimbali katika jamii kuhusu matumizi ya dawa asili katika kupambana na magonjwa yasiyoambukiza kutokana na dawa hizo kuonesha matokeo.

Serikali sasa inahitaji utafiti zaidi katika dawa asilia ili kuweza kupambana na magonjwa hayo kutokana na baadhi ya dawa asili kutumia hata sasa.

“Tunahitaji tafiti zitakazosaidia kutatua changamoto mbalimbali za afya,wakati wa mlipuko wa covid-19 wengi tulirudi kwenye dawa zetu za asili muda umefika sasa tupate majibu ya kisayansi yatakayotuonesha kwenye zile dawa kulikuwa na kemikali gani.

“Aidha tunatambua kuna dawa nyingi sana za asili zinatumika kutibu pumu,shinikizo la juu la damu, saratani na mengineyo hivyo tunawakubusha watafiti na taasisi zetu zote za utafiti kufanya tafiti za dawa hizi ili wananchi wetu wapatiwe taarifa sahihi za dawa hizi,”anaeleza Prof Makubi.

Anasema mchango wa tafiti mbalimbali ni muhimu iwapo utazingatia zaidi ubunifu, ugunduzi wa dawa na chanjo mbal- imbali zitakazosaidia kupunguza magonjwa na vifo vinavyozuilika.

JITIHADA ZA SERIKALI

Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Prof. Mabula Mchembe anasema serikali imefanya maboresho makubwa katika sekta ya afya kwa kuongeza vituo vya afya, maabara kwaajili ya kufanya tafiti za kisayansi na za dawa asilia.

“Serikali imejenga vituo vya afya katika kipindi cha miaka mitano vituo vya afya 17,000 vimejengwa, vifaa na wataalmu wa afya vimeongezwa pia.

“Tunaendelea na kampeni ya madhara ya uvutaji sigara hapa tunatoa elimu kwa jamii kuhusu athari kubwa ya uvutaji wa sigara, tunaendelea kushauri kupunguza unywaji wa pombe ili iwe wa kiasi.

“Wananchi hasa wa mjini hawafanyi mazoezi sio yale ya siku moja wanatakiwa kufanya mazoezi mara kwa mara na pia ulaji wa chumvi nyingi na ile ambayo ni mbichi ni hatari,” anasema Prof. Nchembe.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Huduma za kinga, Wizara ya Afya Dk. Grace Maghembe anasema mpango wa kupambana na magonjwa ya kuambukizwa ulivyozinduliwa mwaka jana umeweza kuongeza nguvu katika kupambana na magonjwa yasiyoambukiza.

“Tumeona kama nchi sasa tuzunguze tuwe na mpango maalum wa kupunguza haya magonjwa kila mwaka Novemba 7 hadi 14 tutakuwa tukiadhimisha maadhimisho haya ya kukabiliana na magonjwa yasi yoambukiza.

“Wananchi wengi hawana uelewa tunataka kuongeza uelewa tunajik- ita kutoa elimu katika vyombo vya habari na maeneo ya mikusanyiko, tunatumia wiki hii kupeana uzoefu kutokana na wataalmu mbalimbali wenye tafiti katika magonjwa yasiyo ya kuambukiza,” anaema.

Anasema mpango huo umeweza kusaidia wananchi kujitokeza na kufanya upimaji wa afya zao kwa hiari na kupata elimu kuhusu jinsi ya kuepukana na magonjwa hayo.

“Wataalamu mbalimbali wanaen- delea kupewa mafunzo ili kuka- milisha mpango huo, kuhamasisha ufanyaji wa mazoezi mara kwa mara, ulaji unaofaa unahitaji kwa kula mlo kamili wananchi waelewe hili hivyo tufanye miili yetu kuwa na mazoezi kulingana na vyakula vinavyotumika,”anashauri Dk Maghembe.

SULUHU LA KUDUMU

Miongoni mwa sababu kubwa zinazotajwa katika kuongezeka kwa magonjwa yasiyoambukiza ni uelewa mdogo wa jamii kuhusu aina ya lishe inayohitajika na ufanyaji mazoezi.

Utaojia wa taarifa zinazokinzana kuhusu afya huenda ikiwa kikwazo katika kukabiliana na magonjwa hayo.

Wataalamu wa afya wanashauri kuwa na kiasi katika kufanya kila kitu kama vile lishe, kazi na mazoezi, lakini je ni wangapi elimu hiyo inawafikia na kuelewa?

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu, Doroth Mwaluko anasema kumekuwa na dhana mbalimbali na mafundisho tofauti kuhusu aina ya lishe inayotakiwa.

“Kwa kiwango kikubwa magonjwa hayo yanahusishwa na mtin- do usiobora kwa maisha ya watu na wamebainisha kwamba hatufanyi mazoezi, ulaji wetu haufai matumizi ya vitu visivyofaa kama tumbaku na unywaji wa pombe uliozidi kiasi.

“Niwaombe na niwe na ujumbe ufuatao mambo mengi yanachangi- wa na chakula lakini kama mdau wa kawaida na mwananchi wa Tanzania tumekuwa na ujumbe mbalimbali kutoka kwa watu mbalimbali kuhusu suala la vyakula bora.

“Huyu atakuambia hiki ni bora na huyu atakuambia hiki sio bora, huyu atakuambia hiki sio kizuri huyu atakuambia hicho hicho kizuri sio kizuri kwahiyo kunad- hana mbalimbali kuhusu masuala ya lishe hivyo niwaombe wahusika mtuelishe ipasavyo ili tule vyakula vinavyofaa kwa wakati mwafaka ili tuondokane na hiyo dhana kwamba hili nalo sio tatizo kumbe ni tatizo,”anasema Mwaluko.

Anasema ufahamu kuhusu lishe ni nafasi kubwa zaidi kushinda magonjwa yasiyoambukiza hivyo ni bora wananchi kufuatilia elimu hiyo.

“Watu wanaohusika na lishe mtujuze vizuri kwa lugha nyepesi ili wananchi wa Tanzania wajue wanakula nini?

Kwa wakati gani? Na kwa mtindo gani? Lakini msisahau kuwa nchi yetu inavyakula vya aina mbalimbali kwahiyo kutumia vyakula hivyo mtupe maarifa mazuri ya kula vyakula vizuri ili tuweze kuepukana na magonjwa yasiyoambukiza yanayotoka na ulaji wetu,”anasisitiza.

Anasema tafiti zinaonesha kuwa kutokuwa na tabia ya upimaji wa afya mara kwa mara huchangia watu wengi kufika hospitali wakiwa wamechelewa.

“Wengi huenda hospitali kupata matibabu pale wanapoona wanashida na niwaombe kuwa tafiti hizi zisaidie kuwafikia wananchi ambao ni wahitaji na waone umuhimu wa kupima vinginevyo tafiti zitaendelea kufanyika kila siku tutaelezwa lakini matokeo na mchango wake utakuwa ni kwa kiwango kidogo.

“Mnaotoa huduma mtoe ipasavyo kuwahudumia wananchi kwa matazamio yao na matarajio yao naamini mtawatendea haki ili waone umuhimu wa kuendelea kupima afya zao na kujikinga ili tufanikiwe kushawishi watu ni wajibu wa watoa huduma kujua lugha nyepesi kwa wananchi ili waweze kuelimishwa ipasavyo.

“Nafahamu mmesoma sana, mnafahamu miili yetu lakini mtujue vilevile na upokeaji wa hayo mnayoeleza tunamitazamo mbalimbali kutokana na mazingira tuliyonayo mimi ukiniambia mazoezi nitakuambia nafanya kazi nyingi na natoka jasho kwahiyo naona inatosha lakini ni nyinyi mtaona haitoshi mtaniambia nifanye hiki na hiki,”anaeleza Mwaluko.

Anasema kuwa watu wa afya na michezo waone umuhimu na wote waongee lugha moja ili tuweze kukabiliana na magonjwa hayo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
584,000SubscribersSubscribe

Latest Articles