27.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 18, 2024

Contact us: [email protected]

LWANDAMINA KUPATA KIPIMO CHA KWANZA

Wachezaji wa Yanga wakifanya mazoezi chini ya kocha wao, Geogre Lwandamina, yaliyofanyika katika viwanja vya Gymkhana jijini Dar es Salaam juzi
Wachezaji wa Yanga wakifanya mazoezi chini ya kocha wao, Geogre Lwandamina, yaliyofanyika katika viwanja vya Gymkhana jijini Dar es Salaam juzi

Na THERESIA GASPER-DAR ES SALAAM

KOCHA mpya wa Yanga, George Lwandamina, kesho katika Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam, atawaongoza mabingwa watetezi wa Ligi Kuu Bara katika mchezo wa kirafiki dhidi ya JKU ya Zanzibar.

Huu utakuwa mchezo wa kwanza kwa Lwandamina ambaye alichukua mikoba ya Hans van der Pluijm na pia utatumika na uongozi wa klabu ya Yanga kama sehemu ya kumtambulisha kocha huyo raia wa Zambia na benchi lake jipya la ufundi.

Lwandamina atasaidiwa na Noel Mwandila pamoja na Juma Mwambusi, huku kocha wa makipa akiwa Juma Pondamali, meneja ni Hafidh Saleh, Edward Bavu ni daktari wa timu, mchua misuli ni Jacob Onyango na mtunza vifaa ni Mohammed Omar ‘Mpogoro’, wakati mkurugenzi wa benchi la ufundi ni Pluijm.

Aidha, uongozi wa Yanga umepanga mchezo huo kuwa rasmi kumuaga mchezaji wao Mbuyu Twite ambaye amedumu katika kikosi hicho kwa miaka minne tangu atue kwa kishindo mwaka 2012 akitokea APR ya Rwanda.

Twite ambaye ni mzaliwa wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo lakini ana uraia wa Rwanda, ameachwa na wana Jangwani hao katika usajili huu wa dirisha dogo.

Mchezaji huyo atakumbukwa kwa kituko alichowahi kufanya baada ya kusaini Simba Julai 2012 mjini Kigali, Rwanda akiwa mchezaji wa APR, lakini siku chache baadaye akasaini na Yanga kama mchezaji wa St. Eloi Lupopo ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).

Mchezo huo ambao utakuwa wa kwanza kwa kocha Lwandamina, ni sehemu ya maandalizi kuelekea mzunguko wa pili wa ligi unaotarajiwa kuanza Desemba 17.

Mchezo huo pia utatumika kupima wachezaji wapya waliosajiliwa kwenye dirisha dogo akiwemo kiungo mkabaji Mzambia, Justice Zulu.

Habari zilizotoka ndani ya klabu hiyo zilieleza kuwa kocha ameamua kuchagua timu hiyo (JKU) ili kupima uwezo wa wachezaji wake baada ya kufanya mazoezi kwa muda mrefu.

“Kabla ya kuanza kwa ligi kocha Lwandamina ameona ni vema kucheza mechi ya kirafiki ili kufahamu mapungufu ambayo bado yapo kwenye kikosi na kuyafanyia kazi mapema,” zilieleza habari hizo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles