NA SHABANI MATUTU, DAR ES SALAAM
MGOMBEA urais wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Waziri wa zamani, Edward Lowassa, leo anatarajiwa kuzungumza na wanawake wa makundi mbalimbali nchini katika kongamano lililoandaliwa na Baraza la Wanawake Chadema (Bawacha).
Mwenyekiti wa Bawacha, Halima Mdee, aliwaambia waandishi wa habari Dar es Salaam jana kuwa Lowassa atazungumza na wanawake hao kupitia televisheni mbalimbali zitakazorusha tukio hilo moja kwa moja.
Alisema katika mkutano huo mgombea huyo wa Ukawa atawaeleza mipango atakayoifanya akipata dhamana ya kuwa rais wa awamu ya tano baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu.
“Katika mkutano huo, Lowassa atazungumza na makundi ya watu wenye ulemavu, wachuuzi, mama lishe, wagonga kokoto, wauza baa, wafanyakazi wa saluni, waandishi wa habari, wasanii wa kike, wanaharakati, viongozi wa Bawacha, wabunge, mabalozi, wanawake wa nchi mbalimbali, walimu, wainjilisti, mahajati, wauguzi, wauza mitumba, wanavyuo wa kike, ‘madada poa’ na wengineo,”alisema Halima.
Mwenyekiti huyo wa Bawacha alielezea kuwa lengo la kongamano hilo ni kuwaunganisha wanawake wa makundi hayo waweze kushiriki kwa ukamilifu katika uchaguzi huo.
“Kama mnavyofahamu idadi ya wanawake nchini ni asilimia 52 kwa mujibu wa takwimu za sensa ya mwaka 2012 ya Watanzania wote, ambao ni zaidi ya nusu. Tunafahamu kundi hilo ndilo lenye zaidi ya asilimi 58 ya wapiga kura waaminifu, hivyo Bawacha ina wajibu wa kutumia haki yao ya katiba ya kupiga kura kwa maslahi mapana ya Taifa,” alisema Halima.
Alisema kaulimbiu ya mkutano huo itakuwa “Lowassa na hatma ya changamoto za wanawake Tanzania” ikiwa na lengo la kuleta mageuzi makubwa katika maisha ya wanawake Tanzania.
Kongamano hilo ambalo Lowassa atafuatana na mkewe, Regina, ni mwanzo wa uzinduzi wa kampini pana zitakazofanywa na Bawacha nchi nzima zitakazojumuisha kanda 10 na kuongozwa na wajumbe wa Kamati Kuu, wabunge na kundi maarufu la 4U Movement.