24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Lowassa ataka Kura zihesabiwe kwa mikono

Pg 2NA SHABANI MATUTU, DAR ES SALAAM

MGOMBEA urais wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) anayeungwa mkono na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Edward Lowassa ameitaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), kusitisha kuhesabu kura kwa kutumia Teknolojia ya Tehama na badala yake zihesabiwe kwa mikono.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Lowassa alisema jaridhishwi na mwenendo wa matokeo ya kura za urais unavyotolewa na kueleza kuwa ukusanyaji huo wa matokeo umekuwa ukikipendelea Chama Cha Mapinduzi (CCM).

“Baada ya kugundua kwamba njia ya Tehama inayotumiwa imekuwa ikichakachuliwa na kuongezewa kura zinazombeba mgombea wa CCM, Dk. John Magufuli, tunaitaka NEC itumie njia ya kuhesabu kwa mikono,” alisema Lowassa.

Njia ya kuhesabu kwa mikono imewahi kutumiwa mwaka 2000 katika Jimbo la Florida, Marekani baada ya kutokea kwa mgogoro wa kutoamini Tehama na kushauriwa kuhesabu kwa njia hiyo.

Katika kinyang’anyiro hicho aliyekuwa mgombea urais wa Chama cha Republican, George Bush, alishinda baada ya kuruhusiwa na Mahakama Kuu kufanyika hivyo, ili kuondoa sintofahamu ya kura zake kuwa karibu na zile za mpinzani wake Al Gore.

Lowassa alisema iwapo NEC itawapuuza na kuendelea na kuhesabu matokeo, umoja huo utatoa kauli nyingine kuhusu hatua watakazozichukua.

Alisema hayupo tayari kupokea matokeo yanayotangazwa na NEC, yanayohusisha madiwani, wabunge na rais kwa sababu yamevurugwa kwa kushirikiana kati ya CCM na tume hiyo.

“Matokeo hayo yameonesha kuwa na nia ya kumbeba Dk. Magufuli kwa sababu kumekuwa na maneneo mbalimbali ambayo kura zinazotangazwa zimekuwa zikitofautiana na matokeo halisi yaliyobandikwa vituoni,” alisema Lowassa.
Aliongeza kuwa pamoja na viongozi wa Ukawa kuelezea matatizo yaliyojitokeza katika uchaguzi huo na kutoa tamko la kutaka kusitishwa lakini NEC wamepuuza na kuendelea kutangaza matokeo, hali inayoonyesha wamepanga kumbeba mgombea wa CCM.

Alisema jambo jingine lililokuwa likionesha kupangwa kwa uchakachuaji wa matokeo hayo ni hatua ya kuwakamata wataalamu wa Ukawa waliokuwa wakikusanya na kujumlisha matokeo katika kituo cha chama hicho.

JUMA DUNI

Naye Mgombea Mwenza wa Chadema, Juma Duni Haji alisema CCM imepenyeza kura hewa zaidi ya milioni 1.6.
“Hiyo ndiyo imechangia kupatikana kwa kura feki katika sehemu mbalimbali ikiwamo majumbani na ndani ya magari ambazo zililenga kuingizwa kwenye matokeo ya uchaguzi,” alisema Duni.

Mgombea mwenza huyo alisema sababu za kukamatwa na polisi kwa wataalamu wao wa Tehama, ililenga kupenyeza uchakachuaji wa kuingiza kura hewa ambazo hawakutaka zibainike.

Duni alitolea mfano wa nyongeza za wizi huo na kusema eneo la Mkuranga Dk. Magufuli aliongezewa kura 1,000 na Chalinze kura 100 huku jimbo la Namtumbo Lowassa alipata kura zaidi ya 47,000 lakini aliandikiwa kura 700.

Mgombea mwenza huyo alisema hatua watakayochukua ni kuishtaki Tume ya Uchaguzi kwa wananchi kuhusu kuporwa ushindi huo.

Sumaye

Naye kampeni meneja wa mgombea huyo, Frederick Sumaye alisema tangu mwanzo wamekuwa na taarifa zinazohusisha kuwapo kwa mfumo usiokuwa rasmi unaopitisha kura za wizi.

Alisema hali ya sintofahamu ilianza kujitokeza baada ya kutokea malalamiko ya kuwepo kuzagaa kwa fomu za kura huku NEC ikishindwa kutolea ufafanuzi.

“Upo uwezekano kwamba, NEC huenda wamezidiwa na wajanja au inawezekana wameshiriki katika wizi huo wa kura ambao unafanywa na CCM. Haki ikipokonywa siku zote huleta matatizo,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles