NA SHABANI MATUTU, DAR ES SALAAM
MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais mstaafu Jakaya Kikwete, amefichua mbinu za chama hicho kushinda uchaguzi mbalimbali ukiwamo uchaguzi Mkuu.
Kikwete alifichua moja ya mbinu hizo jana kwenye kumbukumbu ya aliyekuwa mbunge wa Mbinga Magharibi na mwimbaji maarufu wa CCM, marehemu Kapteni John Komba.
Alisema Komba alikuwa mtu wa aina yake kwa kuwatumia wasanii mbalimbali wa muziki na mwenye ushawishi kwa wapiga kura.
“Wapo wapiga kura ambao walitupigia kura baada ya kuona msanii wanayempenda amepanda jukwaani kwetu kutumbuiza.
“Hali hiyo iliwafanya kutupigia kura kwa sababu wamemuona msanii wanayempenda anatukubali,” alisema Kikwete.
Alisema kwa kutumia mbinu hiyo na nyingine CCM ilijikuta ikiendelea kuwaangusha wapinzani kila uchaguzi unapotokea.
“Wapinzani wamekuwa wakijitahidi kutuangusha lakini wanashindwa kutokana na mbinu zao kuwa dhaifu, mwisho wanajikuta wakiishia kukasirika,” alisema Kikwete.
Mwenyekiti huyo wa CCM akimzungumzia Komba, alisema alikuwa rafiki yake mkubwa tangu wakiwa jeshini na alikuwa mchango mkubwa kwa CCM.
Kikwete alitumia fursa hiyo kuzindua kitabu cha historia ya Marehemu Komba kilichoandikwa na mwandishi Yusuph Halimoja, kikijulikana kama ‘Maisha ya Mzalendo’.
Lengo la mauzo ya kitabu hicho ni kusaidia kupatikana Sh milioni 200.
“Naamini Watanzania hawana utaratibu wa kusoma ila kutokana na ukaribu wangu na marehemu, nitasaidia kutafuta fedha nyingine kwa kuandaa harambee ili shule iweze kujengwa,” alisema Kikwete.
Kikwete alisema atahakikisha anasimama pamoja na familia hiyo ya marehemu Komba kujenga shule hiyo inayotarajiwa kujulikana kama John Komba Primary & Secondary School itakayojengwa Kiromo, Bagamoyo.
Alisema kiwanja hicho kilinunuliwa kutokana na malipo ya nyimbo za mwisho za marehemu Komba, ambayo alikuwa akiidai CCM.