30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

JPM: Nitawatumbua

Magufuli+PHOTONa Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

RAIS John Magufuli amesema waziri au kiongozi yeyote wa serikali atakayewakwamisha wafanyabiasha wanaowekeza katika viwanda, atatumbuliwa mara moja.

Mkuu huyo wa nchi alitoa kauli hiyo  Dar es Salaam jana wakati wa sherehe za utoaji tuzo za Rais kwa wazalishaji bora viwandani kwa mwaka 2015.

Rais Magufuli aliwataka wafanyabiashara  watakapokwama au kukwamishwa na waziri au katibu mkuu yeyote wasisite kumwambia ili awatumbue.

“Mkikwama kokote au kukwamishwa na waziri yeyote au katibu mkuu mtashindwa kuniambia kuwa huyu hafai na kesho yake anaondoka?

“Nataka nchi ya viwanda halafu awepo mtu wa kukwamisha viwanda, he will go (ataondoka).  Nilivyokuwa naimba nataka nchi ya viwanda sikuwa kichaa, sasa aje akwamishe mtu he will go…I can assure you (nawahakikishia)…nataka nchi ya viwanda,”alisema Rais Magufuli.

Alisema kama kuna makosa ambayo yalifanyika miaka iliyopita ni lazima kama serikali wabadilike na kwamba wanaotaka kuwekeza kutoka ndani na nje ya nchi wajitokeze.

“Na ndiyo maana nazungumza ndugu zangu kama makosa tuliyafanya kwenye viwanda tukaacha kutoa motivating agent kwa viwanda vilivyokuwa vimeanzishwa kwa nchi yetu ni lazima tubadilike.. sisi kama serikali na ndiyo maana nawahikikishia yaliyopita si ndwele tugange yaliyopo na yajayo.

“Wanaotaka kuwekeza waje wawekeze kutoka nje na ndani ya nchi; waje wawekeze free without corruption (kwa uhuru bila rushwa) kwa sababu corruption ni kansa na njia ya kupambana ni kuukata, kama uko kwenye mguu ni kuukata haraka.

“Kama kuna mabolozi hapa waleteni wawekezaji tunataka tu-move mbele for development of this country(kwa maendeleo ya nchi hii). Tunataka kujenga nchi kupitia viwanda… tutafanikiwa kujenga uchumi wa nchi yetu,”alisema Rais Magufuli.

Alisema dhambi kubwa  inayowatafuta Watanzania ni roho ya wivu kuanzia serikalini kwa vile mtu anapotaka kuwekeza anapigwa vita.

“Lazima tuseme ukweli, sisi Watanzania sijui tumepewa roho ya aina gani, tunaonekana tuna wivu sana, si ndani ya Serikali si ndani ya wafanyabiashara.

“Yaani kiongozi wa Serikali unamwona mtanzania mwenzako anataka kuwekeza unampiga vita kweli!  Lakini anakuja mtu mwingine kutoka nje unampa, halafu hupati faida hii … ndiyo dhambi tuliyonayo watanzania.

“Ndugu zangu mimi nimekaa serikalini miaka 20 ninafahamu, ninachokisema ni cha ukweli.

“Sasa huu moyo wa kuoneana wivu na kutokuamini kwamba Watanzania wanaweza hiyo ni dhambi kubwa.

“Tuiondoe, mtu akitaka kuwekeza kwenye mbolea aendelee, akitaka kuwekeza kwenye gesi aendelee, akitaka kuwekeza kwenye dhahabu aendelee…,” alisema.

Alisema kwa muda mrefu wameaminika watu kutoka nje kuliko Watanzania huku rushwa ikitamalaki.

“Tumeamini mno watu kutoka nje kuliko sisi wenyewe na huo nao ni ugonjwa, na ugonjwa huo mkubwa tunao sisi ndani ya Serikali. Tunakwamisha humu weee…tunazungumza weee na saa nyingine rushwa ndiyo inatendeka mle,” alisisitiza.

Alisema amekwisha kuwaeleza watendaji wake serikalini na wanafahamu msimamo wake, hivyo wafanyabiashara watoe ushirikiano kuwekeza katika viwanda.

“Ninafahamu changamoto mnazozipata, hata mimi napata changamoto nyingi kweli kweli, ukigeuka hivi unakutana na wafanyakazi hewa, ukigeuka hivi unakutana na wanafunzi hewa!” alisema.

Alieleza masikitiko yake kwa kitendo cha alizeti kulimwa   nchini lakini mafuta yanayotumika ni ya kutoka nje.

“Tuweke maslahi ya taifa letu kwanza, kama kuna alizeti inalimwa hapa Tanzania tujenge kiwanda cha alizeti badala ya kununua mafuta kutoka nje.

“Hapa ukijenga kiwanda cha alizeti uta-create employment.  Si kwamba sitaki bidhaa kutoka nje lakini tuna-balance na ukweli lazima ubaki kuwa ukweli.

“Tulikuwa tuna kiwanda cha matunda kule Tanga, mashine zote zikang’olewa… ninaambiwa zikapelekwa Msumbiji, siwachukii Wanamsumbuji lakini matunda ya Tanga pale yanaoza.

“Rais Kiir wa South Sudan (Sudan Kusini) alipokuja hapa akasema anahitaji kweli unga wa mahindi na mahindi kwa ujumla lakini kinachofanyika nchi jirani inakuja na kununua mahindi na kusaga halafu  inayasaga na kuyapeleka South Sudan kwa bei ya juu zaidi.

“Hivi wafanyabisahata wa Tanzania kwa nini hatusagi na kupelekea moja kwa moja South Sudan nayo tumeshindwa? Na mahindi yako hapa hapa yanalimwa kule Songea halafu wanakuja wafanyabiashara kutoka nje wanayasaga na kuyauza kwa bei ya juu,”alisema.

Alisema Arusha kilikuwapo kiwanda cha maziwa lakini maziwa yamekuwa yakisafirishwa kwenda nje ya nchi na baadaye kurudishwa tena nchini.

“Tulikuwa na kiwanda cha maziwa tukakiuza, maziwa yale ya ndugu zangu wamasai yanasombwa yanapelekwa nchi jirani wanaya-process halafu yanarudi hapa kwetu na sisi tunayanunua. Kwa nini tusingeadd value sisi ya maziwa yetu tukawauzia?” alisema.

Alimtaka Waziri wa Viwanda na Biashara kuhakikisha  viwanda   nchini vinalipishwa kodi kidogo lakini wale wanaokuja kuwekeza kutoka nje walipe kubwa zaidi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles