24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Joto la uteuzi wabunge laanza kupanda Dodoma

Nape-NnauyeNa Bakari Kimwanga, Dodoma

JOTO la uteuzi wa mwisho la kupata wagombea ubunge kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) limezidi kupanda, huku chama hicho kikitangaza uamuzi mgumu kwa wagombea waliocheza rafu na hata kupindua matokeo.

Mbali na hayo, viongozi wa ngazi ya wilaya na mikoa wanaodaiwa kuwabeba kinyume na utaratibu nao wapo hatarini kuvuliwa nyadhifa zao.

Taarifa kutoka ndani ya CCM zililiambia MTANZANIA jana kuwa kikao cha Sekretarieti kilichokutana mjini hapa, kilijadili baadhi ya taarifa na rufaa za wagombea, huku wengine wakiwalalamikia wenzao pamoja na viongozi kwa kucheza rafu wakati wa uchaguzi wa kura za maoni.

Miongoni mwa jambo ambalo limekuwa likizua mjadala, ni hatua ya baadhi ya wabunge kupata kura nyingi katika maeneo yao kinyume na idadi halisi ya wanachama wa CCM kwenye jimbo husika.

Moja kati ya majimbo ambayo wagombea walilalamikia hatua hiyo, ni Jimbo la Iramba ambapo Juma Kilimbah ambaye alikuwa ni moja ya wagombea, alisema pamoja na kura kupigwa bado kura alizopata mgombea mwenzao, Mwigulu Nchemba ni tofauti na idadi ya wapiga kura.

Alidai wakati wa mchakato huo, baadhi ya viongozi wa CCM akiwemo msimamizi wa uchaguzi, walikuwa wakigawa kadi kinyume na utaratibu kwa lengo la kumwezesha Mwigulu kushinda.

Akizungumza mjini hapa, Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alisema vikao hivyo vilivyoanza jana vinaweza kutengua ushindi wa wagombea hao.

Alisema wamepokea malalamiko mengi kuhusu ukiukwaji wa kanuni za uchaguzi katika upigaji wa kura za maoni.

“Pamoja na uchaguzi kumalizika ni lazima wana CCM watambue kuwa kulalamika pembeni au katika vyombo vya habari hakusaidii, ni lazima wafuate utaratibu wa chama.

“Kikubwa wanachama wawe watulivu na vikao hivi vitachambua kwa kina kila tukio katika kila jimbo, wilaya na hata mkoa kabla ya kuteua jina la mgombea wa ubunge kwenye jimbo husika,” alisema Nape.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles