24 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Fanyeni tafiti zitakazowasaidi wakulima-Prof. Tumbo

Na Ramadhan Hassan, Dodoma

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Profesa. Sizya Tumbo, amewataka wafiti nchini kufanya tafiti ambazo zitawasaidia wakulima kuweza kujua masoko ya bidhaa zao zipo wapi.

Pia, amevitaka Vyama vya Ushirika kutumia mapendekezo yanayotokana na tafiti mbalimbali zinazofanywa na wataalamu ili kutatua changamoto zinazovikabili vyama hivyo ili kuleta mabadiliko chanya katika utendaji.

Akizungumza leo Jumanne Machi 16, mwaka huu jijini Dodoma wakati akifungua kongamano la kwanza la Tafiti za Vyama vya ushirika liliandaliwa na Tume ya Maendeleo ya Ushirika nchini(TCDC) ambalo lililowakutanisha viongozi wa vyama vya ushirika kutoka Mikoa yote nchini, Naibu Katibu Mkuu huyo aliwataka watafiti hao kufanya tafiti zenye tija kwa Taifa ikiwemo kujua masoko ya bidhaa mbalimbali yanapatikana wapi.

Naibu Katibu Mkuu huyo amesema wamekuwa wakipokea tafiti mbalimbali kutoka kwa watafiti nchini lakini akadai bado kuna changamoto ya kupata tafiti ambazo zinawasaidia watu wa maisha ya kawaida kujua masoko yapo wapi ya bidhaa zao.

Hivyo, amewataka watafiti hao kujikita zaidi katika tafiti za kujua masoko ya baadhi ya bidhaa yapo wapi ili kuwasaidia wakulima.

Aidha, Prof. Tumbo amesema  sekta hiyo ya ushirika nchini ni muhimu katika kuinua uchumi wa wananchi wasiokuwa na mitaji mikubwa walioamua kuweka nguvu na rasilimali zao.

Amezitaja  baadhi ya changamoto hizo kuwa ni pamoja na ukosefu wa mitaji, viongozi kutokuwa waaminifu, matumizi hafifu ya toknolojia, idadi ndogo ya wananchama, uchache wa wanachama wanawake na vijana, elimu Duni ya ushirika, vyama kutokuwa na mpango mkakati wa kibiashara pamoja na watendaji wasiokuwa na sifa stahiki.

“Tafiti hizi ambazo zimekuwa zikifanywa na vyuo vya elimu na mafunzo na watu binafsi zimekuwa zikitoa mapendekezo ya namana bora ya kuzishuhulikia changamoto za vyama vya ushirika hivyo zisiwekwe kwenya makablasha na mataba kama ilivyokuwa imezoeleka.

“Tafiti hizi zinazofanywa na wadau zisiishie kwenye makablasha, machapisho mbalimbali na kuwekwa kwenye maktaba, bali hakikisheni  zitasaidia kuinua utendaji na kuondoa changamoto zinazoikabili sekta ya Ushirika hivyo niwasihi Tafiti hizi zilete suluhisho katika matumizi sahihi ya Teknolojia ya kisasa katika uendeshaji na usimamizi wa shughuli za vyama vya Ushirika,”amesema Prof. Tumbo.

Hata hivyo ametoa fursa kwa wadau mbalimbali kufanya Tafiti hapa nchini zinazohusu vyama vya ushirika ambapo watatakiwa kuziwasilisha kwa lugha ya Kiswahili ili iwe rahisi kuleta tija .

Kwa upande wake Mrajisi Mkuu wa Vyama vya Ushirika hapa nchini, Dk. Benson Ndiege, amesema lengo la kongamano hilo la siku tatu ni kutoa fursa ya watafiti pamoja na wadau wa maendeleo ya ushirika kukutana na wanachama ,viongozi na watendaji wa vyama vya Ushirika ili kujadiliana kuhusiana na tafiti mbalimbali zilizofanyika.

‘’Matarajio mengine ni kupata mambo mbalimbali yatakayoibuliwa na washiriki ambayo yatatolewa ushauri wa kufanyiwa kazi na Tume ya maendeleo ya Ushirika Tanzania na wadau wengine wa maendeleo ya ushirika,’’amesema  Dk. Ndiege

Sambamba na hayo amebainisha  malengo ya tume katika kuimarisha udhibiti wa vyama vya ushirika ni kuwa na wanachama wenye uelewa na weledi wa kutosha kwenye masuala ya Ushirika, kuwa na uongozi  bora, uwajibikaji.

Nae, Meneja Mkuu wa mradi wa pamoja wa vyama vya Ushirika wa Tumbaku Tanzania, Bakari Hussein, amesema kuwa elimu bado ni changamoto kwa wananchama hivyo kuna haja ya Serikali  kutenga fedha kwa ajili ya kupatiwa elimu ya mara kwa mara.

Pia, amesema kuwa Serikali ichukulie uzito suala la kutumia lugha ya Kiswahili huku akiziomba taasisi za kifedha kupunguza masharti kwao ili waweze kuendesha shughuli zao hususani kutafuta masoko na kupata pembejeo kwa ajili ya wanachama.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles