30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

DC Nkasi apiga marufuku bandari bubu

Na ESTHER MBUSSI-NKASI

MKUU wa Wilaya ya Nkasi, Said Mtanda, amepiga marufuku matumizi ya bandari bubu wilayani humo na kuwataka watumiaji wa bandari hizo kutumia bandari rasmi ya Kapili.

 Alisema Bandari ya Kipili, imefanyiwa ukarabati na Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) kwa shughuli zote za bandari huku hivyo watu waache kutumia bandari bubu ya Kirando ambayo haina ofisi za taasisi muhimu za Serikali ikiwamo Mamlaka ya Mapato (TRA).

Mtanda ambaye alikuwa kwenye operesheni maalumu ya kutembelea bandari bubu wilayani humo, aliahidi kufanya operesheni maalum kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama  kuzuia matumizi ya bandari bubu zote.

Akizungumza na waandishi wa habari wilayani Nkasi, mkoani Katavi, Mtanda alisema Bandari ya Kipili imejikamilisha kwa ofisi na miundombinu ikiwamo ya barabara.

“Baada ya uboreshaji huu kukamilika, bandari yetu imekuwa ya kisasa, hivyo ni wakati muafaka kwa wanaofanya shughuli za bandari kuanza kuitumia na kuachana na bandari bubu zinazozunguka Wilaya ya Nkasi.

“Tutafanya operesheni maalum kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama, tutakaowakamata wanatumia bandari zilizopigwa marufuku tutawachukulia hatua za kisheria,” alisema Mtanda.

Akiwa katika bandari bubu ya Kirando, Mtanda alisema TPA wamebaini bandari bubu 45 zilizopo wilayani humo na zitakazorasimishwa ni tano na nyingine zitafungwa ili kuongeza ufanisi wa mamlaka.

Awali Meneja wa Bandari ya Kigoma, ambaye anasimamia bandari zote za Ziwa Tanganyika, Ajuaye Msese, alisema bandari hiyo haikuwa na barabara na  eneo la kuegesho magari hali iliyokuwa inasababisha usumbufu kwa watumiaji.

Alisema tayari eneo hilo limeshafanyiwa ukarabati hivyo wafanyabiashara na wenye vyombo vya usafiri, wanapaswa kuanza kufanya shughuli zao eneo hilo lenye usalama.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles