30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

DC ATAHADHARISHA MIHURI FEKI CHAPA YA MIFUGO

Na JUDITH NYANGE-MAGU


MKUU wa Wilaya ya Magu mkoani Mwanza, Khadija Nyembo, amewatahadharisha watumishi wa Serikali kupitia idara ya mifugo wilayani humo ambao wametengeneza mihuri bandia kwa ajili ya kupiga chapa mifugo ya wananchi wa wilaya hiyo kwa bei nafuu zaidi tofauti na ile inayotozwa.

Akizungumza jana wakati wa ufunguzi wa  upigaji chapa mifugo, Nyembo alisema amepokea taarifa zisizo rasmi kuhusu uwapo wa baadhi ya watumishi wa  idara ya mifugo wasio waaminifu  ambao wamepanga kuwadanganya wafugaji  kwa kuwatoza gharama nafuu ili waweze kuipiga chapa mifugo yao.

“Watumishi hao  wanatengeneza mihuri  yao isiyo rasmi kwa ajili ya kuipiga chapa mifugo ya wananchi kwa bei nafuu, mfano mwananchi alitakiwa atoe Sh 100,000 lakini wao wanamtoza fedha kidogo  tofauti na bei atayotozwa katika zoezi rasmi halafu wanampigia  mifugo yake chapa.

“Sisi mihuri yetu yote imetengenezwa sehemu moja na tuna alama zetu, tukikubaini umepigiwa  chapa kwa kutoa hela kidogo, basi  wewe na huyo mtaalamu ambaye amekupigia chapa sheria itachukua mkondo wake tutakuweka ndani, kuna malalamiko kuwa baadhi ya wenyeviti wa vitongoji wanaingiza mifugo kutoka maeneo mengine tukikugundua tutakushughulikia pia,” alisema Nyembo.

Nyembo alisema kukamilika upigaji chapa kutasaidia kujulikana idadi sahihi ya mifugo ya wilaya hiyo, upangaji wa matumizi sahihi ya ardhi pamoja na kudhibiti magonjwa yaanayoweza kuenezwa endapo mifugo hiyo itaendelea kutoka sehemu moja kwenda nyingine bila utaratibu rasmi.

Kwa upande wake, Mfugaji wa Kijiji cha Mwaburenga, Juma Ilwagasa,  aliiomba Serikali kuwaongezea muda kwa ajili ya kufanikisha zoezi hilo kwa sababu ni gumu na mifugo iliyopo katika wilaya hiyo ni mingi hivyo muda huo hautatosha.

Naye Merdad Mabinza, alisema utaratibu huo ni mzuri kwa kuwa utasaidia utambuzi wa mifugo yao lakini zoezi hilo litakuwa na changamoto kama Serikali haitaweka utaratibu wa kuendelea kuwapiga chapa ndama ambao watazaliwa baada ya zoezi hilo kukamilika.

Upigaji chapa mifugo wilayani Magu unatarajia kuzifikia ng’ombe  166,320 na utahitimishwa Desemba 31, mwaka huu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles