24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Daktari asimamishwa kazi kwa rushwa

Kassim MajaliwaNa Florence Sanawa

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa, ameagiza kusimamishwa kazi kwa Dk. Fortunatus Namahala wa Kitengo cha Upasuaji katika Hospitali ya Mkoa wa Mtwara (Ligula), kutokana na tuhuma za kumdai mgonjwa rushwa ya Sh 100,000.

Majaliwa alitoa agizo hilo jana, wakati wa kikao cha watumishi wa hospitali hiyo alichokiitisha baada ya kutembelea hospitali hiyo na kupokea malalamiko kutoka kwa wagonjwa na ndugu wa wagonjwa.

Akiwa njiani kuelekea wodi aliyopangiwa kuiona, Waziri mkuu alikutana na kundi la wagonjwa waliokuwa wakiimba. “Tuna jambo, tuna jambo” wakiashiria kutaka kusikilizwa.

Mwananchi mmoja Tatu Abdallah limweleza waziri mkuu kero ya rushwa, ambapo alilazimika kuuza shamba ili kunusuru maisha ya baba yake aliyefukuzwa hospitalini hapo kwa kukosa fedha.

“Februari mosi, nilimleta baba yangu hapa nikaambiwa anatakiwa kufanyiwa upasuaji. Nikaandikiwa ninunue dawa za Sh 85,000 hapo nje (pharmacy).

“Lakini pia daktari akasema anataka Sh 100,000 ya kwake nilimpa hizo fedha, lakini hadi Februari 7 hakufanyiwa huo upasuaji.

“Februari 12, mwaka huu  baba alitolewa wodini na kuambiwa arudi Februari 16. Niliumia sababu kijiji tunachotoka ni mbali na hali ya baba ilizidi kuzorota.

“Ndipo baba akaniambia nirudi kijijini kwetu Kilomba nikauze ekari 2.5 za shamba lake ili tulipie gharama za matibabu. Niliuza na kumpeleka baba katika Zahanati ya Sajora. Huko nililipa Sh 560,000 na baba akafanyiwa upasuaji sasa hivi yuko nyumbani.

“Leo nataka huyu daktari aje achukue boksi hili la dawa alizoniandikia na pia anirudishie hela yangu iliyopotea bure, ni kwa nini aliniandikia wakati baba hajampa huduma yoyote?,” alisema. Alipoulizwa kama anaweza kumtambua daktari huyo akimwona, mama huyo alikiri kuwa anaweza kumtambua.

Waziri mkuu alitembelea pia wodi ya akina mama waliojifungua na kukuta wakiwa wametandikiwa shuka moja na wagonjwa kulazimika kuweka kanga juu ya mipira wanayolalia wodini wanayonunua wenyewe.

Akiwa katika kikao na watumishi hao, waziri mkuu aliwainua madaktari wote ili wajitambulishe ndipo akamwomba mama aliyedaiwa rushwa aende kumshika mkono daktari mhusika.

“Gwaride la utambuzi ni jambo la kawaida. RPC hakikisha huyu mama hasumbuliwi. Naanza na huyu daktari kwa sababu rushwa haivumiliki. “Katibu Tawala (RAS) simamia suala lake lakini pia shirikiana na TAKUKURU na polisi kufanya uchunguzi wa jambo hili hadi mwisho,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles