28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

CRDB yazindua huduma mpya ya SimBanking iliyoboreshwa

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Benki ya CRDB imezindua huduma ya SimBanking iliyoboreshwa kuwawezesha wateja kupata huduma za kisasa na kufikia malengo yao ya kifedha.

Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dk. Faustine Ndugulile (wa pili kushoto), akizindua huduma mpya ya SimBanking inayowawezesha Watanzania kufungua akaunti popote walipo kupitia simu ya mkononi, uzinduzi huo umefanyika jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa programu hiyo iliyoboreshwa na kupewa jina la ‘Benki ni SimBanking’, Mkurugenzi Mtendaji wa benki hiyo, Abdulmajid Nsekela, amesema inawawezesha wateja kuwa na uwanja mpana wa kupata huduma za kifedha kama vile kufungua akaunti kwa njia ya kidijitali, maombi ya mkopo, malipo ya bili na malipo ya bima.

“Kwa kupakua programu iliyoboreshwa ya SimBanking, mtu yeyote anaweza kufungua akaunti ya benki popote alipo bila gharama. Tunaamini programu hii mpya itachangia kuimarisha mfumo wa kifedha wa nchi yetu.

“Programu hii imeundwa kwa kutumia teknolojia ya kisasa na tutajumuisha pia mfumo wa Mamlaka ya Udhibiti wa Bima Tanzania (TIRA) ili kuwezesha wateja kupata stika za kidijiti kupitia programu hii mara baada ya kufanya malipo,” amesema Nsekela.

Naye Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dk. Faustine Ndungulile, ameipongeza Benki ya CRDB kwa kubuni na kuanzisha bidhaa na huduma zinazoharakisha utekelezaji wa mipango ya kitaifa ya uchumi na maendeleo inayoendeshwa na serikali.

Dk. Ndugulile amewahimiza Watanzania hasa wale wa vijijini kutumia Programu ya SimBanking iliyoboreshwa kufungua akaunti za benki na kuanza kufurahia huduma za kibenki.

“Kwa kuwa sasa tuna njia rahisi ya kufungua akaunti ambayo haiitaji kutembelea tawi, naamini programu iliyoboreshwa ya SimBanking itatusaidia kujumuisha watu wengi katika mfumo rasmi wa kifedha,”amesema Dk. Ndugulile.

Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dk. Faustine Ndugulile (wa pili kushoto), akionyesha SimBanking mpya inavyoonekana baada ya kujiunga wakati wa uzinduzi wa huduma hiyo, uliofanyika jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela wa pili kulia ni Naibu Mwenyekiti wa Bodi ya Benki ya CRDB, Profesa Neema Mori na kulia ni Naibu Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA), Khadija Said.

Mabadiliko ya kidijiti yanaendelea kuwa sehemu muhimu ya mkakati wa Benki ya CRDB unaoendelea wa miaka mitano (2018 – 2022), na programu mpya ya SimBanking ni sehemu ya mkakati wa benki hiyo uliolenga kuwapa wateja suluhisho la huduma za kibenki.

SimBanking ilianzishwa kwa mara ya kwanza mwaka 2011 kuwawezesha wateja wa Benki ya CRDB kupata huduma za kibenki kwa ukaribu na kwa miaka mingi SimBanking imekuwa huduma ya kuaminika zaidi kwenye soko.

Wanachotakiwa kufanya wateja ni kupiga *150*03# au kupakua CRDB SimBanking Playstore au Appstore na kupata huduma za kibenki zilizoboreshwa zaidi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles