23.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 16, 2024

Contact us: [email protected]

Bundi atua Yanga

NA ADAM MKWEPU, DAR ES SALAAM

KUELEKEA katika mchezo wa Kombe la  Shirikisho Afrika  dhidi ya Medeama ya Ghana, timu ya Yanga imeendelea kukumbwa na majanga kwa  baadhi ya wachezaji wake tegemeo baada ya winga, Deus Kaseke, kupata  ajali  ya pikipiki jana eneo la Ubungo akiwa anaelekea mazoezini Uwanja wa Boko Veterani, jijini Dar es Salaam.

Tukio hilo lilitokea saa 9:15 asubuhi, wakati mchezaji huyo akitokea nyumbani kwake Kigogo, hivyo kufanya idadi ya wachezaji watano majeruhi wa timu hiyo wengine wakiwa ni Geofrey Mwashiuya, Juma Mahadhi, Malimi Busungu na  Haji Mwinyi.

Hali hii inaonyesha kuwa kuna bundi mbaya ametua Jangwani, kwani mbali na majeruhi hao mshambuliaji Mzimbabwe, Donald Ngoma, anasumbuliwa na malaria huku Obrey Chirwa na Nadir Harub ‘Cannavaro’, wakiomba ruhusu  baada ya kupata matatizo ya kifamilia.

Akizungumza na MTANZANIA jana, daktari wa timu hiyo, Edward Bavu, alisema kwamba  hali  ya winga huyo inaendelea vizuri  baada ya kupata  matibabu kwa michubuko aliyopata katika mwili wake.

“Kaseke anaungana na wachezaji wengine majeruhi, Mwashiuya na Mwinyi bado wanasumbuliwa na maumivu ya goti wakati jana Mahadhi alijitonesha jeraha lake alilopata katika mchezo wa TP Mazembe uliochezwa Juni 28 jijini Dar es Salaam,” alisema Bavu.

Wakati huo huo, katika kuhakikisha kuwa haipotezi mchezo wake ujao,  Kocha Mkuu wa Yanga, Hans Van der Pluijm, amepanga kutumia video ya mchezo kati ya TP Mazembe na Medeama uliochezwa Kongo, kuwamaliza Medeama.

 

Yanga inayotarajia kuweka kambi Mwanza, itaivaa Medeama Julai 16 mwaka huu, mchezo unaotarajiwa kuwa na mvuto zaidi kutokana na mechi hiyo kuwa kama fainali kwa Yanga kwa kuwa imeshapoteza mechi mbili za Kundi A.

 

Pluijm ataitumia video hiyo kuangalia mapungufu ya Medeama katika mchezo huo ambao Mazembe waliibuka na ushindi wa mabao 3-1.

 

Taarifa ndani ya Yanga zinasema kuwa, Plujim anahaha kuweka mambo sawa ambapo alilazimika kutuma ujumbe wa watu kuangalia mchezo huo na atatumia makosa hayo kama njia mojawapo ya kufanya vizuri katika mchezo ujao.

 

Yanga imepoteza michezo miwili ya Kundi A, ikianza kwa kufungwa na Mo Bejaia ya Algeria bao 1-0 na kufungwa tena bao 1-0 na TP Mazembe katika mchezo uliochezwa katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles