27.5 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

BRELA yatoa tuzo kwa Wabunifu

Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital

Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) imetoa tuzo kwa Wabunifu sita wa Kitanzania ikiwa njia mojawapo ya kutambua mchango wao katika ukuaji wa sekta ya biashara na afya nchini.

Judith Kadege Mjumbe kutoka Bodi ya Ushauri ya Brela akiongea na washiriki katima maadhimisho ya siku ya miliki ubunifu katika kituo cha mikutano cha kimataifa cha Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es Salaam

Tuzo hizo zimetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara, Dk. Hashil Abdallah kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, katika maadhimisho ya Siku ya Miliki Bunifu Duniani iliyofanyika Aprili 28, 2023 katika ukumbi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Tuzo ya kwanza ilienda kwa Eliot Company Ltd. mfanyabiashara mwenye Alama ya Biashara ya Active Mama ambapo bidhaa yake ilisajiliwa mwaka 2018 na bidhaa yake imekaa sokoni kwa miaka saba sasa na imesambaa katika mikoa 26. Hadi sasa amefanikiwa kutoa ajira kwa watu 25.

Tuzo ya pili ilienda kwa mmiliki wa kampuni ya Natureripe Kilimanjaro Ltd. Mfanyabiashara mwenye alama ya biashara ya Natureripe iliyosajiliwa mwaka 2006 na imekaa sokoni kwa miaka 23.

Bidhaa hizo kwa sasa zinapatikana ndani na nje ya nchi ya Tanzania kama vile Dubai, Qatar, Australia, Uingereza na ameweza kutoa ajira kwa watu 43. Kampuni hiyo pia imefanikiwa kutunza mazingira kwa kupanda miti na kutumia mabaki yanayotokana na malighafi zilizotumika kwa ajili ya kuboresha mazingira kwa maendeleo endelevu.

Tuzo ya tatu imetolewa kwa, Emmanuel Mushi akiwa ni Mbunifu aliyetumia Miliki Ubunifu (Hataza) kwa ajili ya kusaidia jamii. Mushi alivumbua Automatic Modified Neonatal Incubator iliyosajiliwa mwaka 2020. Vumbuzi yake imesaidia kuwakuza watoto njiti 2,000.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara, Dkt. Hashil Abdallah(aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na viongozi pamoja na Washiriki wa Siku ya Miliki Ubunifu Duniani waliopata tuzo na vyeti kutokana na Bunifu mbalimbali tarehe Aprili 28, 2023 Katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa (JNICC) Dar es Salaam.

Uzinduzi wa kifaa chake ulifanyika na Taasisi ya Costech 2019. Hataza yake hadi sasa inatumika katika mkoa wa Manyara.

Tuzo ya nne imetolewa kwa kampuni ya LAMATA Village Entertainment inayoongozwa na Bi. Leah Mwendamseke maarufu kwa jina la LAMATA. Tuzo yake imetambulika kama mbunifu aliyewawezesha wengine kupitia Miliki Ubunifu kwa kutoa ajira kwa watu 100 na kukuza kipato kupitia filamu ya Jua Kali.

Tuzo ya tano imetolewa kwa Fahamu Sheria Foundation kwa ubunifu wa kuwa na mfumo wa Sheria Kiganjani. Amesajili alama ya biashara mwaka 2021 na amefanikiwa kutumia aina mbili za Miliki Ubunifu ambazo ni Alama za Biashara na Hatimiliki.

Mawanda ya umiliki umejikita katika kulinda alama za biashara na taarifa za TEHAMA. Bunifu zao zimejikita katika kutoa huduma kwa watu wa kipato cha chini na wamefanikiwa kuwafikia watu mbalimbali wakiwa na malengo ya kufikia watu milioni mbili.

Tuzo ya Sita imetolewa kwa mmiliki wa kampuni ta NN General Supplies yenye alama ya biashara ya HQ. Kupitia bidhaa zake, imesaidia jamii kwa kusambaza taulo za kike kwa bei nafuu.

Dk. Abdallah amewapongeza wabunifu waliopata tuzo na na kusisitiza kuwa tuzo hizo ziwe chachu ya kukuza ubunifu katika biashara ili wengine waone umuhimu wa kuendeleza na kukuza ubunifu katika shughuli za kibiashara na maisha ya kila siku.

BRELA itaendelea kuhamasisha wafanyabiashara kusajili Alama za Biashara na Huduma na wavumbuzi kupata Hataza ili kazi zao ziweze kulindwa kisheria.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles