23.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 16, 2024

Contact us: [email protected]

Benki ya Twiga yafilisika

benno_nduluNA EVANS MAGEGE

BENKI Kuu ya Tanzania (BoT) imechukuwa uamuzi wa kuisimamia Benki la Twiga (Twiga Bancorp Limited) kwa sababu ya upungufu wa mtaji hatua ambayo inaifanya benki hiyo isiweze kujiendesha tena.

Uamuzi huo wa BoT umeanza mara moja jana kwa kuvunja Bodi ya Wakurugenzi na Menejimenti ya Benki ya Twiga Bancorp Limited, ili kupisha meneja mpya aliyeteuliwa na BoT ambaye atakuwa na jukumu la usimamizi na uendeshaji wa benki hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari jana katika ukumbi wa mikutano wa BoT jijini Dar es Salaam, Gavana  wa BoT, Profesa Benno Ndulu, alisema uamuzi wa kuisimamia Benki ya Twiga Bancorp Limited umechukuliwa baada ya kubaini kuwa benki hiyo ina upungufu mkubwa wa mtaji kinyume na matakwa ya sheria ya mabenki na taasisi za fedha ya mwaka 2006.

Alisema upungufu huo wa mtaji unahatarisha usalama wa sekta ya fedha na pia benki hiyo kuendelea kutoa huduma za kibenki kutahatarisha usalama wa amana za wateja wake.

“Kwa mamlaka niliyopewa chini ya kifungu cha sheria namba 56(1)(g)(i) na 56(2)(a)-(d) cha Sheria ya Mabenki  na Taasisi za Fedha ya mwaka 2006, Benki Kuu ya Tanzania imeamua kuchukua usimamizi wa Benki ya Twiga Bancorp Limited kuanzia Oktoba 28. Tayari nimevunja Bodi ya Wakurugenzi na Menejimenti yote, nimeteua Meneja mpya kwa ajili ya usimamizi, lakini  uamuzi huo haujawagusa wafanyakazi wa chini labda inawezekana katika mabadiliko mapya ikatokea wakaguswa.

“Benki hii inamilikiwa na Serikali kwa asilimia 100, lakini tangu kuanzishwa kwake imekuwa na tatizo la mtaji, kwa mujibu wa sheria yetu benki yoyote inatakiwa kuanza ikiwa na mtaji usiopungua Sh trilioni 7.5 na benki hii ilianza kwa mtaji huo lakini hadi sasa imebakiza mtaji wa Sh bilioni 21 tu. Pamoja na matatizo ya mtaji benki hii ina mali zenye thamani ya Sh bilioni 90 ukitoa Sh bilioni kama tisa hivi zenye matatizo, Sh bilioni 81 ziko salama,” alisema.

Aliongeza kwamba pamoja na BoT kuchukuwa uamuzi huo, watu wote wanaodaiwa na benki hiyo wasidhani wako salama, kwani wataendelea kuwafuatilia ili warejeshe madeni wanayodaiwa.

Gavana Ndulu alitumia nafasi hiyo kuuarifu umma kwamba ndani ya takribani wiki moja kuanzia jana, shughuli za utoaji wa huduma za kibenki kwa Benki ya  Twiga Bancorp Limited zitasimama ili kutoa nafasi ya kupanga taratibu za uendeshaji wa benki hiyo.

“Isieleweke kwamba tunataka kukaa pale moja kwa moja, sisi tupo kwa muda tu na tunawaalika wawekezaji waje kuwekeza katika benki hii….BoT inapenda kuuhakikishia umma kuwa itaendelea kulinda masilahi ya wenye amana katika mabenki kwa lengo la kuleta ustahimilivu katika sekta ya fedha,” alisema.

Uamuzi huu wa BoT umekuja wakati ambako Rais Dk. John Magufuli, aliwahi kutoa agizo la kuangalia uwezekano wa kuifunga kutokana na kujiendesha kihasara.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles