28.4 C
Dar es Salaam
Sunday, April 28, 2024

Contact us: [email protected]

Bashe aita wawekezaji sekta ya kilimo

Na Esther Mnyika, Mtanzania Digital

Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe amewataka wawekezaji kuja kuwekeza nchini kwani kuna fursa nyingi na kwa ajili ya kumsaidia mkulima mdogo ili kuweza kufanya kilimo chenye tija na kulifanya Bara la Afrika kujitegemea kwenye chakula hata yanapotokea majanga Duniani.

Akizungumza Septemba 5, jijini Dar es Salaam kwenye kikao kilichowakutanisha mawaziri wa kilimo na mifugo na uvuvi kutoka bara na visiwani pamoja na wadau wa sekta hiyo kwenye mkutano Jukwaa la Mfumo ya Chakula Afrika (AGRF) kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Julius Nyerere (JNICC).

Amesema Tanzania imeweka mazingira mazuri kwa ajili ya uwekazaji.

“Ili mkulima aweze kuzalisha kwa tija anahitaji mbengu bora, kuwa na uhakika wa mbolea kwa wakati na kwa gharama nafuu lakini pia miundombinu ya maji ili aweze kuzalisha mara mbili mpaka tatu kwa mwaka,” amesema Bashe.

Amesema changamoto kubwa ni mitaji lakini pia uhakika wa mkulima kwenye kile anachokilima hivyo wawekezaji wanapaswa kuweka mitaji yao ili kusaidia sekta hiyo kwani Serikali imetenga ardhi ya kutosha kwa Kituo cha Uwekezaji (TIC) kwa ajili ya uwekezaji.

“Tumekutana hapa mawaziri wa kilimo na mifugo na uvuvi ili kuwaonyesha wawekezaji maeneo ya kuwekeza ili kuboresha sekta hii kwani sasa hivi kilimo ni biashara na ndio maana tumefungua milango kwa mkulima kuuza mazao yake popote pale,” amesema.

Ameongeza kuwa kupitia mkutano huo wa AGRF wataonyesha dunia fursa zilizopo nchini katika sekta ya kilimo ili kuhakikisha nchi inalima kwa tija lakini pia inaacha utegemezi wa chakula na badala yake inauza kwenye mataifa mengine.

Waziri wa Fedha, Dk. Mwigulu Nchemba.

Naye Waziri wa Fedha, Dk. Mwigulu Nchemba amesema kujikita kwenye sekta ya kilimo kutasaidia kupunguza ukosefu wa ajira kwa vijana lakini pia kupunguza kutumia pesa nyingi kuagiza chakula kutoka nje.

Amesema kilimo sasa imekuwa sekta ya biashara hivyo inapaswa kutumiwa ili kubadilisha maisha ya vijana kwani nchi inaenda kujitegemea katika chakula lakini pia kuzalisha ajira nyingi hali itakayochochea kuzalisha walipakodi wengi.

“Idadi ya watu wanaohitaji ajira ni kubwa, hivyo juhudi za Serikali ni kuingiza vijana wengi na wanawake kwenye sekta ya kilimo kwani sasa hivi kilimo kimekuwa biashara hivyo mapato ya serikali yataongezeka ikiwa sekta hii itakua na kuwekezwa ili izalishe kisasa,” amesema Mwigulu.

Kwa upande wake Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega amesema ili kuboresha sekta ya kilimo,uvuvi na mifugo teknolojia,masoko na mitaji inahitajika hivyo wawekezaji wanapaswa kuwekeza ili kukuza sekta hiyo kuweza kuzalisha kwa tija na kuuza nje.

“Asilimia 70 ya mahitaji ya mifugo yametokana na mazao ya kwenye kilimo hivyo wizara hizi mbili tunategemeana huu mkutano ni fursa kwa nchi na wananchi,” amesema Ulega.

Mkutano wa Jukwaa la mfiumo ya chakula Afrika AGRF unaofanyika jijini Dar es Salaam umeanza Septemba 5 hadi 8 ambapo unahudhuliwa na watu zaidi ya 3,000 wakiwamo marais sita wa nchi tofauti za Bara la Afrika wakiongozwa na Rais wa Tanzania Dk. Samia Suluhu Hassan.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles