Na JENNIFER ULLEMBO-DAR ES SALAAM
KUELEKEA katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara kati ya Simba na Azam FC, uongozi wa wanalambalamba umejipanga kuwadhibiti wapinzani wao, Â licha ya kumiliki wachezaji wenye ubora zaidi msimu huu.
Azam na Simba zinatarajiwa kupambana Jumamosi kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.
Simba msimu huu imesajili wachezaji wanne wa kikosi cha kwanza kutoka Azam, ambao ni aliyekuwa nahodha John Bocco, Aishi Manula, Shomary Kapombe na Erasto Nyoni, hivyo kufanya mchezo huo kuwa mgumu zaidi.
Akizungumza na MTANZANIA jana, Ofisa Habari wa Azam FC, Jaffar Idd, alisema inafahamika wazi kuwa, wapinzani wao watakuwa wamejipanga kuhakikisha wanaendeleza rekodi yao ya ushindi, lakini ni vema wakajua kuwa matokeo yanaweza kubadilika.
Idd alisema kwa kikosi cha Azam kinaendelea kujifua kwa kasi zaidi, ili kufanikisha lengo la kushinda mchezo huo, hivyo Simba wasitegemee kupata ushindi kiurahisi.
Simba ilianza msimu huu kwa ushindi mnono wa mabao 7-0 dhidi ya Ruvu Shooting, wakati Azam iliifunga Ndanda bao 1-0.
Msimu uliopita, mzunguko wa kwanza Simba ilishinda bao 1-0, lililofungwa na Shiza Kichuya, wakati mzunguko wa pili Azam iliifunga Simba bao 1-0, lililofungwa na John Bocco.