Na Ramadhan Hassan, Dodoma
WAZIRI wa Maji Jumaa Aweso ameutaka Mfuko wa maji kuweka utaratibu mzuri wa kuwalipa ya wakandarasi na kuacha ubabaishaji pindi ambapo malipo yao yanapokuwa yamekamilika.
Akizungumza jana jijini hapa wakati wa utiaji saini mikataba 86 ya ujenzi wa miundombinu ya maji yenye thamani ya Sh bilioni 309.99, Waziri Aweso amesema Wizara yake inategemea na wakandarasi hivyo hakuna haja ya kuleta ubabaishaji katika miradi ya maji hivyo ameomba malipo yao yanapokamilika wapewe ili waweze kutimiza kazi walizopewa.
“Mfuko wa maji wekeni mfumo mzuri na nitaufumua na kuweka utaratibu mzuri ili mtu akiwasilisha hati ya malipo apewe fedha aende kufanya kazi, baadhi ya wakandarasi wananyanyasika kama kuna malipo anastahili kulipwa alipwe,” amesema Aweso.
Hata hivyo, ametaka kuwapo na ushirikishwaji wa wananchi na wabunge katika kutekeleza miradi hiyo.
“Wewe Mkandarasi unatakiwa kushirkiana na Mbunge unapopeleka vifaa wasilina na mbunge sio kimya kimya tu maji ni zaidi ya kila kitu kwenye majimbo yetu,” amesema.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa RUWASA, Mhandisi Clement Kivegalo amesema wamepanga kutekeleza miradi 1,527 ambapo kati ya hiyo miradi 351 ilikuwa ya utafutaji wa vyanzo vya maji na usanifu wakati miradi 1,176 ni miradi ya ujenzi wa miundombinu
Mhandisi Kivegalo amesema kuwa sehemu ya miradi 1,176 ni miradi ambayo imeibuka mwaka wa fedha uliopita ambayo ni 317 huku miradi mipya ni 462 wakati miradi ya ukarabati na upanuzi ilikuwa 397.
“Hali ya utekelezaji wa miradi hiyo, miradi 317 iliyovuka mwaka, miradi 249 imekamilika na inatoa huduma ya maji wakati miradi ile 397 ya ukarabati na upanuzi ambayo inatekelezwa kwa mfumo huku miradi 301 ikikamilika na kutoa huduma ya maji,” amesema Mhandisi Kivegalo.
Ameongeza kuwa, katika miradi iliyopita 462, miradi 138 ilitangazwa makao makuu ya RUWASA ili kupata wakandarasi na miradi 324 ilitangazwa na mameneja wa mikoa 25 kwa kutumia bodi za uzabuni.
Naye, Mbunge wa Morogoro Kusini Mashariki, Hamis Taletale amemshukuru Waziri na Ruwasa kwa kumsaidia kuweza kupata miradi miwili ya maji ambayo itaondoa tatizo la wakazi wa Jimbo hilo kutembea umbali mrefu.