23.6 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Ataka kujiua kwa sumu ya mahindi baada ya wazazi kuingilia mahusiano yake

Na Ashura Kazinja, Morogoro

Mkazi wa Magoweko wilayani Goweko mkoani Morogoro, Secilia Ching’unyau (22) amenusurika kifo akijaribu kujiua kwa kunywa sumu ya kuhifadhia mahindi aliyoichanganya na pombe aina ya Vodka-Cuca kwa madai ya wazazi kutaka kuvunja mahusiano kati yake na mpenzi wake.

Akizungumzia tukio hilo leo Januari 27, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, (SACP) Fortunatus Muslim, amesema tukio hilo limetokea Januari 14, saa moja usiku katika mtaa wa Magoweko Tarafa na Wilaya ya Gairo, ambapo alijaribu kujiua kwa kunywa sumu ya kuhifadhia mahindi aina ya Acteric, huku kiini cha tukio hilo kikiwa ni wivu wa kimapenzi kuwa wazazi wanaingilia kuvunja mahusiano na mpenzi wake.

“Inaelezwa mtuhumiwa alikunywa sumu hiyo kwa kuchanganya na pombe aina ya Vodka-cuca, ambapo alikutwa amelewa na kupoteza kumbukumbu huku akiwa ameegemea ukuta wa nyumba na pembeni yake kukiwa na vikopo viwili vya pombe aina ya Vodka/cuca vikiwa vimeshatumika na vikopo viwili vyenye kuhifadhia mahindi aina ya Acteric ambavyo vilikuwa bado havijatumika.

“Mtuhumiwa amelazwa katika Kituo cha Afya Gairo akiendelea na matibabu na kwamba hali yake inaendelea vizuri,” amesema Kamanda Muslim.

Katika tukio lingine Jeshi la polisi mkoani Morogoro limewakamata madereva zaidi ya 1,000 mkoani humo kwa kosa la kukutwa na madeni ya faini za makosa ya barabarani.

Akizungumzia tukio hilo Kamanda Muslim amesema madereva hao wamekamatwa katika msako uliofanywa na jeshi la polisi wa kukamata magari na madereva wanaodaiwa faini za makosa ya barabarani ulionza tarehe 18 mwezi huu.

‘’Upande wa madeni oparesheni hii inafanyika nchi nzima, sio tu mkoa wa Morogoro, kukamata magari na madereva wanaodaiwa faini za makosa ya usalama barabarani, hapo mwanzo madereva walikuwa wakikamatwa walitakiwa kulipa faini zao hapohapo, lakini wengi walilalamika eti hawana pesa na wengine wanaenda kulipa mbali, ndipo serikali ilipoweka mfumo wa dereva kupewa siku saba,’’ alisema Kamanda Muslim.

Aidha, amesema mbali na serikali kuweka mfumo wa dereva anayefanya makosa ya usalama barabarani kulipa ndani ya siku saba lakini bado kuna madereva wanakamatwa kwa kutolipa madeni yao na kusababisha kazi ya kuwatafuta ambapo mpaka sasa wameshakamatwa madereva 1384.

Amewataka madereva wote wanaodaiwa faini hizo kulipa, na kwamba hakuna dereva anayedaiwa atakayepita mkoa wa Morogoro, kwani wamejipanga vizuri kuhakikisha yeyote anayedaiwa anakamatwa na analipa madeni yake.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles