Na MANENO SELANYIKA–DAR ES SALAAM
MKAZI wa Mwananyamala kwa Manjunju, Dar es Salaam, Amina Maige, amehukumiwa kwenda jela miaka miwili na kulipa faini ya Sh 500,000 baada ya kupatikana na hatia ya kumtesa, kumjeruhi aliyekuwa mfanyakazi wake wa ndani, Yuster Kashinde.
Mshtakiwa pia amepewa adhabu ya kumlipa mlalamikaji Sh milioni mbili kama gharama alizotumia mlalamikaji kutibiwa maumivu ya vidonda alivyomsababishia.
Hukumu hiyo ilitolewa jana na Hakimu Caroline Kiliwa wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kinondoni hiyo baada ya kujiridhisha na ushahidi uliowasilishwa mahakamni hapo na upande wa mashtaka.
“Kwa mazingira hayo Mahakama hii inakutia hatiani kwa kosa hilo kutokana na ushahidi wa kina uliowasilishwa hapa na mashahidi wanane wa upande wa mlalamikaji,” alisema Kiliwa.
Hakimu alisema shahidi namba moja ambaye ni Yuster aliiambia mahakama kwamba majeraha aliyoyapata yalisababishwa na mshtakiwa.
Alisema mahakama ilithibitisha majeraha hasa sehemu ya sikio la kushoto ambalo liliharibiwa kabisa.
“Utatumikia kifungo cha nje miaka miwili kwa usimamizi wa maofisa wa ustawi wa jamii hivyo uwe makini.
“Endapo utapatikana na kosa la jinai kabla ya kumaliza kifungo hiki adhabu itabadilika kwa mujibu wa sheria,” alisema.
Katika utetezi, Wakili wa Amina, Emmanuel Muga, aliiomba mahakama isimpatie mteja wake adhabu kali kwa kuwa ni kosa la kwanza na hajawahi kupatikana na shtaka la jinai.