NA JESSCA NANGAWE
STAA wa muziki wa BongoFleva, Ali Kiba, ameingia kwenye rekodi mpya baada ya wimbo wake mpya alioupa jina la ‘Seduce Me’ kuvunja rekodi, baada ya kutazamwa na watu zaidi ya milioni 2 kwenye mtandao wa ‘You tube’ ndani ya siku tatu.
Kiba alichia wimbo wake huo Ijumaa iliyopita na kupokelewa kwa ukubwa wa aina yake na wapenzi wa muziki wa ndani na nje ya Tanzania.
Kiba anakuwa msanii wa pili Afrika kufikisha idadi hiyo kubwa ya watazamaji ndani ya muda mfupi, akitanguliwa na msanii wa Nigeria, Ayodeji Balogun, maarufu Wizkid kufikisha watazamaji zaidi ya milioni moja katika kipindi cha siku tatu, baada ya kuachia wimbo wa ‘Came Closer’, aliomshirikisha mkali wa miondoko ya hip pop wa nchini Marekani, Drake.
Kabla ya Kiba, rekodi hiyo kwa hapa nchini ilikuwa inashikiliwa na mkali mwingine wa muziki wa Bongo Fleva, Naseeb Abdul, maarufu kama Diamond, ambaye mwaka jana alifikisha watazamaji milioni moja ndani ya siku nne kupitia wimbo wake wa ‘Kidogo’, aliolishirikisha kundi la P Square la Nigeria.
Kiba alitumia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Instagram kuwashukuru mashabiki wake kwa kuendelea kumsapoti baada ya kuachia wimbo huo, ambao mwenyewe amedai hakutegemea kama ungefanya vizuri kama ilivyotokea.
“Asanteni sana kwa upendo wenu mashabiki zangu, hii ina maana kubwa sana kwangu, mbarikiwe sana, kwa kuwa ninafanya hivi kwa ajili yenu, ninawapenda sana,” alisema Kiba.
Wimbo Seduce Me ulioimbwa na Kiba umekwenda sambamba na ule wa kundi la Wasafi Classic, linalomilikiwa na mpinzani wake, Diamond, ambalo hivi karibuni liliachia video yao wimbo wake mpya
unaojulikana kwa jina la ‘Zilipendwa’.
Wimbo huo pia umeonekana kutingisha anga za muziki wa Bongo Fleva, ambapo mpaka sasa una watazamaji zaidi ya milioni moja.
Kwa muda mrefu Kiba na Diamond wamekuwa na upinzani mkali katika kazi zao za muziki, huku kila mmoja akijinadi kumfunika mwenzake.
Upinzani wa wasanii hao pia umewagawa wapenzi wa muziki nchini kiasi cha kuibuka makundi mawili hasimu, moja likijiita ‘Team Diamond’ na jingine likifahamika kama ‘Team Kiba’.