26.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Ali Kiba adhihirisha ubabe kwa Wizkid

wizkid-alikiba

Na CHRISTOPHER MSEKENA

BRING back our award! Ndiyo neno la Kimombo lililokuwa maarufu zaidi kwa siku mbili hizi katika mitandao ya kijamii, baada ya Ali Kiba kutakiwa kupewa tuzo yake badala ya Wizkid ambaye alitangazwa awali kuibuka kidedea.

Kwa Kiswahili rahisi sentesi hiyo inamaanisha: “Rudisha tuzo yetu!”

Wizkid alitangazwa mshindi na kupewa tuzo ya Best African Act 2016, iliyoandaliwa na MTV Europe Music Awards (MTV EMA) huko Rotterdam,  Uholanzi, kabla ya kutenguliwa na kutakiwa kurejeshewa Mbongo Fleva, Ali Kiba ambaye ameshinda kihalali.

Awali, kupitia mitandao kura zilionyesha wazi kuwa Kiba alistahili ushindi kutokana na kuwa na kura nyingi, lakini baadaye waandaaji wakampa tuzo Wizkid jambo ambalo Kiba na team yake walilalamikia.

Kiba akiwa msanii pekee anayetoka Afrika Mashariki katika tuzo hizo, alikuwa akishindana katika Kipengele cha Msanii Bora Afrika ‘Best African Act’ akiwa na wakali wengine kama Black Coffee, Casper Nyovest (Afrika Kusini), Olamide na Wizkid wa Nigeria.

Mbele ya mastaa wakubwa wa dunia, Wizkid alitangazwa  mshindi wa tuzo hiyo, ila ukirudi kwenye kura kupitia mtandao wao unaonyesha wazi Kiba ndiye mshindi.

 WIZKID ALIANDALIWA KUWA MSHINDI

Msanii gani hivi sasa Afrika ana kiki unyamwezini na kwingineko duniani? Jibu ni Wizkid. Hakuna msanii yeyote Afrika anayefikia kasi ya kijana huyu katika kuufikisha muziki wa Afrika kwenye levo za kidunia.

Cheki kazi zake alizofanya na Drake, Chris Brown, Trey Songz na French Montana utabaini ana spidi kali kama ile ya 4G.

Amewahi kusikika akisema muziki wake ni mkubwa kuliko tuzo ndiyo maana huwa haombi kura kama wasanii wengine wanavyofanya.

Muziki wa Afrika umemtengeneza Wizkid kuwa bora na ukionekana unapingana na ukweli huo ni lazima watu watakushangaa.

Mwezi Juni, Wizkid alishinda tuzo ya BET kwenye Kipengele cha Msanii Bora wa Kimataifa kutoka Afrika, tuzo iliyokuwa inawaniwa na Black Coffee, Diamond Platnumz, Yemi Alade, Cassper Nyovest, Mzvee na AKA.

Hakuishia hapo mwezi Agosti, mwaka huu huko Dallas Texas, Wizkid alishinda tena tuzo za AFRIMMA kwenye Kipengele cha Msanii Bora Afrika.

Oktoba 22, Wizkid alichangia kuwarudisha mikono mitupu Watanzania watano waliotajwa kuwania Tuzo za MTV MAMA zilizotolewa huko Afrika Kusini tena kwenye kipengele kilekile cha Msanii Bora wa Mwaka na Msanii Bora wa Kiume zilizokuwa zinawaniwa na Diamond Platnumz.

Wiki iliyopita kabla hajapewa tuzo ya MTV EMA, huko Nigeria Wizkid alitangazwa kuwa mshindi wa tuzo ya Msanii Bora wa Mwaka kwenye tuzo za AFRIMA.

Kwa hiyo unaweza kuona ni jinsi gani Wizkid anavyozidi kujijengea imani kwa waandaaji wa tuzo mbalimbali kuwa yeye ni bora Afrika.

Sasa MTV EMA ni nani mpaka waende kinyume na matokeo ya tuzo nyingi ambazo Wizkid ameshinda kama Msanii Bora Afrika? Kwa presha ya kuonekana watu wa ajabu, tuzo ya Kiba wakampa Wizkid.

NGUVU YA ALI KIBA YAWAUMBUA

Kwenye kipengele hicho jina la Ali Kiba lilikuwa geni kabisa. Mtazame Black Coffee, Cassper Nyovest, Wizkid na Olamide utagundua ni wasanii ambao tayari wametajwa  sana kuwania tuzo mbalimbali zaidi ya Kiba.

Kutoonekana kwa jina lake kwenye tuzo nyingi kuliwapa nguvu MTV EMA wafanye kile walichokifanya bila kujua kuwa ukanda wa Afrika Mashariki, Kiba ni habari nyingine, ana mashabiki wenye mahaba ya dhati juu yake.

Ndiyo maana baada ya uongozi wa Rockstar4000 ulipohoji sambamba na nguvu ya mashabiki kwenye mitandao, MTV EMA wakakiri kutoa tuzo hiyo kwa Wizkid kimakosa.

KIBA AONYESHA UMWAMBA

Mwezi Oktoba, mwaka huu kwenye Tamasha la Mombasa Rocks Music nchini Kenya, wawili hawa walivutana na kupelekea kuvuruga ratiba ya tamasha hilo, kitu kilichofanya Kiba kufanya shoo chini ya kiwango.

Katika shoo hiyo, Kiba na Wizkid walivutana juu ya nani aanze kupanda jukwaani kila mmoja akidai yeye anakubalika zaidi ukanda huo, lakini kwa tuzo hii bila shaka, ubishi utakuwa umekwisha!

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles