27.1 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Ajabu wabunge wanawake kumlilia Clinton

Aliyekuwa mgombea  urais wa Marekani  kwa tiketi ya Democratic, Hillary Clinton
Aliyekuwa mgombea urais wa Marekani kwa tiketi ya Democratic, Hillary Clinton

NA ALOYCE NDELEIO,

UCHAGUZI wa Marekani  lilikuwa ni tukio moja ambalo lilitawala nyanja nzima ya habari hususani baada ya matokeo yake  kutangazwa na  kuibua picha tofauti na matarajio ya walio  wengi.

Aidha wale wanaoegemea kutabiri masuala ya siasa za Marekani walibakia  kuegemea  umaarufu ambao uongozi unaomaliza muda wake  umejipatia  katika Afrika, hawa waliduwazwa; wale wanaoielewa sura ya kinyonga ya Marekani  hawakushangaa kuyaona mabadiliko yaliyotokea.

Kwa upande mwingine  matamanio na matarajio ya  watu na hususani miongoni mwa nchi za Afrika  walikuwa  upande wa Democrat taswira  ambayo inaweza kuelezwa kuwa ni kutokana na kudekezwa na uongozi unaomaliza muda wake na hususani kwa mtazamo wa masuala ya ‘Kwa  hisani ya watu wa Marekani.’

Wale wanaozielewa siasa  za Marekani  ni kwamba haziwezi kushabikiwa kama ligi ya soka ya Ulaya, au kule Marekani kwenyewe katika ligi ya Mpira wa Vikapu ya NBA.

Kilichojitokeza na ambacho kinaweza kuelezwa kuwa  tukio la ajabu ni ile taarifa kwamba  wabunge  wanawake wa Tanzania  wamesikitishwa na kushindwa kwa mgombea  urais wa Marekani  kwa tiketi ya Democratic, Hillary Clinton.

Kauli hiyo  inatosha kuwafikirisha wavuja jasho na kuipata picha halisi kwamba ni upande upi wanawake hao walikuwa wameuegemea katika mtazamo na matamanio yao katika Uchaguzi Mkuu wa Marekani.

Kama  ujumbe huo wa kusikitishwa na matokeo hayo miongoni mwa wabunge wanawake wa Tanzania  ulimfikia  au la, hilo wavuja jasho hawawezi kulifahamu. Lakini kama  ujumbe huo ulimfikia wavuja jasho wanavuta  hisia tofauti.

Kwa mbali hisia  za wavuja jasho zinakutana na mwangwi wa sauti ikisema, “Msinililie mimi enyi wanawake wa Bongo, jililieni wenyewe na muwalilie wenzenu ambao hamuwaungi mkono  katika chaguzi zenu.”

Kwa upande mwingine inaweza kuelezwa kuwa wabunge hao hawajawaona wanawake waliogombea nfasi za uongozi nchini mwao na ambao  huenda walishindwa kutokana na kutoungwa mkono na wanawake wenzao.

Kwa kuangalia uhalisia hali hiyo inaonesha unafiki  uliomo ndani ya wanasiasa wanawake kwa kuwa  katika Uchaguzi Mkuu  wa mwaka jana  wa Rais na wabunge na madiwani  walikuwapo wanawake waliogombea nafasi mbalimbali na hata nafasi ya Urais.

Pamoja na hali hiyo wapo wanawake pia waliotangaza nia na kuchukua  fomu za kugombea nafasi hiyo na hata kufikia hatua za mchujo  ambapo majina yao yalikatwa.

Hoja ni wanawake wangapi  miongoni mwao hadi  leo wameshaonesha kusikitishwa  kushindwa  katika uchaguzi huo kwa wanawake wenzao?

Leo hii wamekuwapo wanawake  ambao  pamoja na  kushinda  uchaguzi  huo  katika ngazi ya ubunge, wapinzani wao  wamefungua  kesi mahakamani kupinga  ushindi wao. Mmojawapo ni Mbunge wa Jimbo la Bunda Mjini, Ester Bulaya  ambaye katika kesi  zilizofunguliwa katika mahakama ngazi tofauti ameshinda kesi yake  dhidi ya mpinzani wake Mzee Steven Wassira.

Hoja ni wanawake wangapi  wameweza kujitokeza hadharani kumlilia katika mapambano yake ya kesi hiyo  na walau hata kumpongeza hadharani kama ambavyo wangetarajia kumpongeza Clinton iwapo angeshinda?

Inapotokea wachambuzi wa mambo wakasema kuwa  baadhi ya akili za wanasiasa  na hata baadhi ya wasomi wetu zimehamishiwa Ughaibuni nani atakataa uhalisia huo kwamba hawaoni yaliyomo ndani  mwao bali kwa wenzao? Je, wabunge hao wanawake hivi kweli walimsikitikia Anna Mghwira  aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya  ACT – Wazalendo kwa kushindwa katika Uchaguzi Mkuu uliopita?

Upo usemi hisani huanza nyumbani  lakini hilo  kwa wanasiasa hao halifahamiki ila lililo muhimu kwao labda ni lile ambalo linatokana na ‘Kwa hisani ya watu wa Marekani.’

Si ajabu kwamba  hivi sasa wapo katika matamanio ya kinjozi kwamba kura hizo zikirudiwa kuhesabiwa Clinton ataibuka mshindi. Haiyumkini hawa wanatakiwa kutoa boriti jichoni ndipo waone vibanzi hivyo vilivyopo Ughaibuni.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles