*Ni wale wanaohitimu mafunzo ya JKT
Na Ramadhan Hassan, Dodoma
JESHI la Kujenga Taifa (JKT) lipo katika mkakati wa mazungumzo na Wizara za Kilimo na ile ya Mifugo na Uvuvi ili kuwaunganisha vijana ambao wamemaliza mafunzo ya JKT na hawana kazi katika mradi wa Building Better Tomorrow (BBT).
Hayo yameelezwa leo Julai 27,2023 na Mkuu wa Jeshi hilo, Meja Jenerali Rajabu Mabele wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Jeshi hilo kwa mwaka 2023-2024 kwa Waandishi wa Habari.
Meja Jenerali Mabele amesema wapo katika mazungumzo na wizara hizo kuhakikisha vijana wanaomaliza Jeshi wanajiunga katika mpango huo.
Amesema kuwa lengo la Serikali ya awamu ya sita ni kuhakikisha vijana wengi wanapatiwa mafunzo na Jeshi hilo ambayo yatawasaidia kuwa na malezi bora ya kizalendo kwa manufaa ya nchi yao.
“Tunamshukuru sana Rais wetu kwa nia ya dhati katika kuliwezesha Jeshi la Kujenga Taifa JKT ambapo bajeti imeongezeka kwa asilimia 54 toka Sh bilioni 3.7 kwa mwaka 2021/2022 hadi kufikia bajeti ya sh bilioni 9.96 kwa Mwaka 2023/2024,” amesema.
Amesema fedha hizo pia zitatumika kuboresha vyuo vya ufundi vya Jeshi hilo kwa lengo la kuwapatia vijana ujuzi na maarifa pale wanapokuwa wanapatiwa mafunzo ili kuweza kujitegemea na kujiajiri.
Pia amesema jeshi hilo limejipanga katika suala zima la uzalishaji ikiwemo kilimo na ufugaji ili Tanzania kuweza kuwa ghala la chakula.
“Sisi kama Jeshi katika mwaka huu wa fedha tumejipanga kujenga miundombinu ya Skimu za umwagiliaji ambapo mradi huo umetengewa jumla ya Shilingi bilioni4 katika kukidhi hitajio la chakula ili nchi iwe na usalma wa chakula,” amesema Meja Jen. Mabele.
Amesema wataongeza idadi ya uzalishaji wa mpunga kutoka ekari 3,000 hadi 5,000 huku mahindi kutoka ekari 6,625 hadi 8,500 na kuweza kupata tani 12,750 na alizeti kutoka ekari 2,115 hadi 6,000.