21.5 C
Dar es Salaam
Saturday, July 27, 2024

Contact us: [email protected]

Watoto wenye siko seli Muhimbili wakabidhiwa msaada wa mahitaji muhimu na Taasisi ya Matha Sangu

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Watoto wanaokabiliwa na ugonjwa wa siko seli wanaopatiwa matibabu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), wamekabidhiwa msaada na Taasisi ya Martha Sangu (Martha Sangu Sickle Cell Foundation), wenye thamani ya Sh 500,000.

Hafla hiyo imefanyika hospitalini hapo mapema leo Jumamosi Februari 13, ambapo imekwenda sambamba na uelimishaji kwa wazazi wanaouguza watoto hao ili kuweza kutambua changamoto zinazowakabili na namna wanavyoweza kuwasaidia vema pindi zinapojitokeza.

Akizungumza na waandishi wa habari, Mkurugenzi wa Taasisi hiyo, Martha Sangu amesema kwamba wamekabidhi sabuni za kufulia, sabuni za kuogea, ‘pampasi’ za watoto, ‘wipes’ na bidhaa nyingine za mahitaji madogo madogo.

“Taasisi yetu inahusika kusaidia misaada mbalimbali, kuelimisha jamii hasa kwa wagonjwa wa siko seli na wazazi (ndugu wa karibu) wanaouguza mgonjwa wa siko seli,” amebainisha.

Ameongeza; “Hivyo leo tumefika hapa na kukabidhi bidhaa hizi, lengo hasa lilikuwa kuwafikia wagonjwa hawa na kutoa elimu kwa wazazi wanaowaugua, ama jamaa zao wa karibu.

“Tunafanya juhudi hizi kuwafikia wagonjwa pale wanapopungukiwa na mahitaji madogo madogo na kupata fursa ya kuwapa elimu wazazi au jamaa zao ili waweze kutambua namna ya kuwasaidia wagonjwa hawa pale inapotokea wamekumbana na ‘crisis’ za ugonjwa huu.

“Crisis’ ni ile hali ambayo hutokea wakati zile seli nyekundu zinakuwa zimeziba njia ya upitishaji damu mwilini na hivyo kumsababishia maumivu makali mgonjwa husika,” amebainisha.

Martha amefafanua “Hivyo, Tunapotoa elimu, wazazi na ndugu hawa wanapata uelewa, jinsi gani ya kumsaidia mgonjwa pale anapokumbana na madhara yatokanayo na ugonjwa huu na au kumuwahisha mapema hospitali kwa msaada zaidi wa kitabibu.

“Tumeona baadhi ya kesi zikitokea kwa watoto wenye ugonjwa huu, ndiyo maana tumependa kuwatembelea hospitalini na kuzungumza na wazazi, jamaa zao,” amesema.

Amesema wanahamasisha pia vikundi vingine visikae nyuma viendelee kujitokeza, kuwaibua wagonjwa na kuelimisha jamii nzima kuhusu ugonjwa huo na mengineyo.

“Sisi tumejikita kumuelimisha mwanamke kwa sababu tunaamini ukimuelimisha mwanamke umeelimisha jamii, tunaomba Serikali iendelee kushirikiana nasi,” amesema.

Pynious Levsom ambaye ni mmoja wa wanachama wa Taasisi hiyo, ametoa rai kwa jamii kujenga utamaduni wa kujitolea kusaidia wengine hata ikiwa ni kwa kile kinachoonekana kwa macho kuwa ni kidogo.

“Tuishi na maneno haya, unaweza usifanye kitu kikubwa lakini ukafanya kitu kidogo kwa upendo mkubwa kwa sababu ukimsaidia mtu, hata kwa maombi yako haupotezi.

“Ukimsaidia mtu unawekeza si lazima uoneshwe hapa ndiyo unalipwa…. utaona malipo yanakuja yenyewe na si tu kwa wagonjwa wa siko seli, changamoto zipo nyingi, kuna watoto yatima, wajane na makundi mengineyo.

“Kama umebaikiwa kitu kitoe, wote tumeumbwa ili tuweze kutengeneza hali zetu za baadae, ukitoa Mwenyezi Mungu atakubariki na kukusaidia pale ulipotoa,” amesisitiza.

Akizungumza, Afisa Muuguzi wa Jengo la Watoto Muhimbili, Rehema Fuko ameishukuru Taasisi hiyo kwa moyo wa upendo walioonesha na kujitoa kwao kusaidia mahitaji hayo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles