23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Watoto, wafu waandikishwa kupiga kura Z’bar

NA SHABANI MATUTU, DAR ES SALAAM
CHAMA cha Wananchi (CUF), kimetoa matokeo ya utafiti wake kuhusu Daftari la Wapiga Kura Zanzibar ikieleza kuwa watoto wasiotimiza umri wa miaka 18 na watu waliofariki dunia, majina yao yanaendelea kutumika katika dafrati hilo huku Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) ikikaa kimya.
Kutokana na hali hiyo CUF kimesema kinashangazwa na hatua ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) kuandaa mipango kinayodai ni ya kuendelea kuhujumu upigaji kura kwa kutumia vyombo vya ulinzi ambavyo hutoa watu kutoka Tanzania Bara.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad, alidai CCM imekuwa ikiandaa njama za hila kwa msaada wa ZEC kuandikisha vijana wasiokuwa Wazanzibari kinyume cha sheria.
Alisema pamoja na hali hiyo, bado kuna haja kwa Wazanzibari kuendelea kushikamana kuhakikisha wanaunga mkono wimbi la mabadiliko Visiwani humo.
“Hivi sasa CCM inatumia kambi za Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) iliyopo Chukwani kuandikisha vijana wasiokuwa Wazanzibari na kuwapatia vitambulisho vya Mzanzibari mkaazi (ZAN IDs) kwa ajili ya kujiandikisha kama wapiga kura.
“Mwaka 2010 niliyasema haya baada ya matokeo ya Uchaguzi na Rais Dk. Ali Mohamed Shein aliahidi kufanya marekebisho ndani ya ZEC suala ambalo halijafanyika hadi sasa,” alisema Maalim Seif
Utafiti
Akitoa matokeo ya utafiti katika mkutano huo jana, Kiongozi wa Kitengo cha Sera, Utafiti na Mafunzo wa CUF Zanzibar, Hassan Jani Masoud, alisema utafiti walioufanya katika majimbo 10 umebaini kuwapo ukiukwaji wa sheria za uchaguzi unaochangia kuipa ushindi CCM.
Alisema daftari la mwaka 2010 linaonyesha kuwa na watu 407,658 waliopiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2010 ambako wapiga kura wengi hawakustahili kubaki katika Daftari la Kudumu.
“Daftari hili la ZEC ikiwa halitafanyiwa marekebisho ni wazi wale wapiga kura waliofariki dunia hivi karibuni wataendelea kuhesabika kama wapiga kura halali na jambo kama hili lilifanyika mwaka 2010.
“Kuna wapiga kura wakazi wa Jimbo la Donge wameandikishwa katika Jimbo la Tumbatu Shehia za Pale na Mto wa Pwani ya kuwa si wakazi wa shehia hizo ambao wanafikia 463 na suala hilo ZEC wanalijua,” alisema Masoud
Mtafiti huyo alisema takwimu za jumla ya wapiga kura kwa Jimbo, za mwaka 2010 kwa majimbo yote ya Pemba na Unguja ukitoa Wawi, wako chini ya 8,507.

Maalim na saikolojia
Wakati huohuo, CUF kimemtaka Rais Dk. Ali Mohamed Shein ambaye ni Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kujiandaa kisaikolojia kukabidhi nchi kwa Makamu wake wa Kwanza wa Rais, Maalim Seif Sharif Hamad.
Akijibu swali katika mkutano huo, Maalim Seif alikiri kwa mara ya kwanza kushindwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010.
“Tukumbuke kwamba kabla ya kufanyika kwa uchaguzi wa mwaka 2010 yalifanyika kwanza maridhiano hali iliyosababisha kufanyika uchaguzi huru, haki na wa amani na hakuna hata nzi aliyebanwa katika kipindi cha kampeni.
Maalim alisema katika uchaguzi huo, CUF waliitaka Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) isimamishe utangazaji wa matokeo kutokana na kubaini kuwapo njama za kuhujumiwa na CCM.
Maalim na urais
Kuhusu suala la yeye kugombea urais katika kila uchaguzi, Maalim Seif alisema CUF kimekuwa kikitoa fursa kwa kila mwenye sifa kuchukua fomu lakini hawajitokezi.
“Si kweli kwamba chama kimekuwa kikiwazuia wanachama wenye sifa kuwania nafasi hiyo au wanachama wa CUF hawana sifa ya kuwania urais, bali kinapokuwa kinatangaza uchukuaji wa fomu huwa hawajitokezi,” alisema.
Serikali ya Umoja
CUF pia kimepinga kukutwa na kile kilichovikuta vyama vya upinzani vya Kenya na Zimbabwe vilivyopigwa mweleka katika uchaguzi baada ya viongozi wake kukubali kuunda serikali ya Umoja wa Taifa.
Akizungumzia suala hilo, Mkurugenzi wa Mambo ya Nje wa CUF, Ismail Jussa Ladhu alisema mazingira ya siasa ya Zanzibar ni tofauti na ya Kenya na Zimbabwe.
“Kwa upande wa Zimbabwe chama cha MDC kilikuwa na mgogoro wa ndani ya chama huku kwa upande wa Kenya, uchaguzi haukuwa huru na haki wakati CUF inabebwa na siasa za ukweli kwa kukosoa waziwazi mambo mazito,” alisema.
Hatua
Akielezea hatua tisa za kuchukua kuzuia machafuko kutokea Zanzabar, Maalim Seif alisema ni kuwataka wote waliopewa vitambulisho vya Mzanzibari kinyume na sheria wavisalimishe na wasiandikishwe kwenye daftari.
Hatua nyingine ni kuwapatia vitambulisho vya Mzanzibari wananchi walio na haki ya kupata kabla ya uandikishwaji wa mwisho unaotarajiwa kuanza Mei 16 hadi Juni 28 mwaka huu, waweze kutumia haki yao ya katiba.
Alimtaka Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Idara Maalumu za SMZ, Haji Omar Kheri, aache kuwatumia wakuu wa Wilaya, Mikoa na Masheha katika usajili wa wapiga kura haramu kwa kuwapatia vitambulisho vya Mzanzibari.
Waziri Kheri aibuka
Akizungumzia madai hayo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Idara Maalumu za SMZ, Haji Omar Kheri, alisema anasubiri kusoma taarifa ya Maalim Seif kabla ya kujibu.
“Suala la ugawaji majimbo lipo chini ya ZEC siyo langu na wala si suala la kusubiriwa mimi, ila hilo la kushutumiwa kuhusu mamluki na kuhusishwa na vikosi maalum vya SMZ nasubiri kuisoma taarifa ya Maalim kisha nami nitajibu,” alisema Waziri Kheri
Alipotafutwa, Mwenyekiti wa ZEC, Jecha Salim Jecha, hakupokea simu na hata alipotumiwa ujumbe mfupi wa simu hakujibu.
CCM yajibu
Akizungumzia tuhuma hizo Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai alisema chama hicho kimechoshwa na lawama za CUF.
“CUF wamekuwa na kawaida ya kupiga kelele kwa mambo wanayokuwa wanafanya, tunajua kuwa wamechukua Wapemba na kuwaleta Zanzibar ili waje kupiga kura na ndiyo maana katika nyumba moja utawakuta wapo hadi 40,” alisema.
Akizungumzia kuhusu kuwamo watoto na marehemu katika daftari la wapiga kura wanaodaiwa kuipigia kura CCM, alisema taratibu za ZEC na sheria zinataka majina yabandikwe kwa wiki moja ili kama kuna shaka ya jina liwekewe pingamizi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles