24.3 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Wanawake walipoamua kuwaadhibu wanaume

Wasanii waigiza igizo la LysistrataNa Markus Mpangala

KARIBU tena wasomaji wa safu hii tuendelee kujisomea kitabu ili kupata burudani, elimu na starehe ya ubongo kwa ujumla. Leo tusome kitabu chetu cha ‘Lysistrata’ kilichoandikwa na Aristophanes karne nyingi zilizopita.

Nianze kwa kutoa mfano. Mara nyingi tumekuwa tukisikia maandamano na migomo ya aina mbalimbali kwenye nchi tofauti. Migomo hii ina sababu zake, na nchi kama Togo na Kenya tulishuhudia migomo ya wanawake dhidi ya wanaume.

Mgomo wa Kenya na Togo ilikuwa na dhamira ileile, kunyima unyumba. Wanawake wa Kenya waliamua kuwanyima unyumba waume na wapenzi kwa madai ya kushindwa kutatua matatizo yanayojitokeza katika nchi zao. Mgomo huo ni maarufu kama ‘Sex strike’.

Leo tusome mwanzilishi wa mgomo huo na jinsi kitabu hicho kilivyoiteka dunia. Aristophanes alitunga kitabu hiki akiwa na dhamira ya kuondoa matatizo katika jamii.

Watunzi na kampuni mbalimbali za vitabu walivutiwa na utunzi huo, hivyo mpaka leo tunachambua hapa, kimechapishwa mara kadhaa. Kitabu cha Lysistrata kilitolewa mwaka 2005, lakini muswada wake uliandaliwa mwaka 2003, ikiwa ni kuboresha mchezo wenyewe.

Lysistrata ni mchezo wa kuigiza uliotungwa kwa lengo la kuwasiliana na jamii na kuonyesha suluhisho la matatizo yanayowakabili wananchi wa Ugiriki na kilitungwa kwa Kigiriki.

Aristophanes alitunga kitabu hiki mwaka 411 BC kuelezea matatizo ya vita yaliyoikumba Ugiriki, hususani vita vya Peloponnesian. Vita hii ilisababisha maafa makubwa kwa wanawake na watoto.

Wanasiasa na viongozi mbalimbali walijishughulisha zaidi na malumbano ambayo yalisababisha kuitumbukiza Ugiriki katika vita.

Aristophanes aliandika mchezo  huu kwa njia ya vichekesho (Comedy) na kuupatia jina hili la Lysistrata. Katika mchezo huo mtunzi huyo anamtumia mwanamke mmoja mzaliwa wa jiji la Athen (Ugiriki).

Mwanamke huyo ni Lysistrata ambaye amechorwa kama mwanamke anayepinga maafa ya Peloponnesia yaliyoharibu jamii.

Katika kutatafuta ufumbuzi wa matatizo, mtunzi wa Lysistrata, Aristophanes anatoa suluhisho kwamba itafika wakati wanawake wataanza kugoma na kuwanyima unyumba wanaume ili watatue matatizo ya nchi. Katika mchezo huo Lysistrata anaanza kuhamaisha wanawake wagome. Mchezo unaanza hivi;- Calonice anaingia jukwaa;

‘Habari yako Calonice? Lysistrata anasalimia

“Oooh! Ni njema pia Lysistrata, lakini unaonekana hauko vizuri? Kulikoni? Mbona umeketi na hawa watu weusi, inakupendeza kweli? Huonekani kuwa furaha, uso unatisha,” anahoji Calonice.

Lysistrata naye anajibu;

“Calonice, ni zaidi ya mzigo mzito ninaoweza kubeba,

Kwanza mimi ni mzuri, navutia kuliko viumbe wote duniani, wanaume wanasema ni watu wa kutamaniwa.

Calonice anajibu, “lakini si kuna ukweli kwa wasemalo?

“Labda kwa wale wanaofanya biashara ya kuuza miili yao. Ni hao wanachezewa vitandani kama mipira ya kona,” anasema Lysistrata

“Rafiki yangu mpenzi, wanaume watakuja tu. Ni vigumu kwa wanawake kuwasaka wanaume, si unajua? Tuna mengi ya kufanya, mume anatakiwa kulelewa na kutendewa mambo mazuri kama mtoto. Mke unakuwa kama kijakazi, kuogesha watoto, kuwapa chakula na kuwavisha,” anasema Calonice

Naam, kwa hapa mwandishi anatuonyesha unyonge wa wanawake. Anajaribu kuonyesha namna gani mwanamke anavyoweza kufikiria matatizo ya mambo yanayomsonga kila siku. Mwandishi anatuonyesha kana kwamba wanawake wamekuwa kitoweo cha mapenzi kwa wanaume.

Lakini baadaye Lysistrata anajaribu kumwelimisha zaidi Calonice. Lysitrata anasema, “Lakini nakwambia, hapo ni sehemu ndogo tu uliyogusa katika uzito wa jambo hili,

Calonice anajibu, “Kwani kuna nini cha zaidi rafiki Lysistrata. Ndiyo sababu ya kufikiria wanawake waunde jeshi lao? Au uzito gani unazungumzia?

“Hakuna mwanamume atakayehusiana na wanawake. Kama hilo likifanyika basi tutaona wanaume wote wakitufuata. Lakini ni uzito mkubwa wa jambo hili,” Lysistrata anazidi kujieleza.

“Nchi yetu imo kwenye machafuko. Mwokozi yuko mikononi mwetu. Lazima mizizi ya vita iondolewe Peloponnesians. Waambie wanawake wote waungane nasi, lazima tusimame na kuwanyima unyumba wanaume wote wa Athens, kuanzia Peloponnesus  na Boeotia. Mkono mwema hutenda meme kwa ajili ya Ugiriki,” anasema Lysistrata.

Mpaka kufika hapo mwanamke mwingine Calonice, ambaye amekuwa mhusika mkuu msaidizi, ameonyesha kuwa yeye ni wmanamke ambaye anahitaji sapoti katika maisha ya kijamii.

Katika zama zetu hizi hususani hapa nchini, Lysistrata angeitwa mchochezi, kwani alifanya kazi kubwa sana kuwachochea wanawake wote wahakikishe wanawanyima unyumba wanaume.

Baadaye tunaonyesha kuwa Lysitstrata anafanikiwa kuwashawishi wanawake wengi mno na kuingia mitaani kuaandamana dhidi ya hali ya machafuko ya Athens. Wanawake wengine ni Myrrhine na Lampito ambao wamechorwa kuwa shujaa zaidi.

“Vidole vyako vifanye kazi kubwa. Najisikia kama ningekuwa mhanga wa vita hii, wangenikoma wanaume,” anasema Lampito.

Mwandishi Aristophanes katika sehemu ya hitimisho la igizo hilo anasema kuwa uzito wa penzi la mwanamke yeyote kwa mwanaume wake ndio utaamua kuwa atamnyima unyumba kama njia ya kushinikiza kutatauliwa kwa matatizo mbalimbali ndani ya nchi.

Leysistrata kwenye mchezo huo anajikuta akisema kama wanaume wanapenda kumfanya aishi kwa raha na starehe basi lazima wachukue hatua za kusikiliza hoja zake, na kama hawataki basi yeye angelikuwa wa kwanza kuendeleza harakati za kunyima kile ambacho wanaume wanakihitaji sana, unyumba.

Lakini maneno yale yalikuwa yakiwagusa waliohusika na machafuko ya Ugiriki, ambapo historia inatuambia kulikuwa na mapigano makubwa nyakati hizo.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles