27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Sera ya Elimu Bure inavyowatesa Wakenya

CLASS TWO STUDENTS1284889194MICHAEL MAURUS NA MITANDAO

KENYA imekuwa ikitajwa kuwa miongoni mwa nchi za Afrika zinazotoa elimu bora, japo wapo wanaopinga hilo, wakiwamo baadhi ya Watanzania.

Wanaoisifia Kenya kielimu, wanadai kuwa Wakenya wamekuwa na uelewa wa hali ya juu katika mambo mbalimbali kutokana na msingi uliojengwa katika elimu yao kuanzia ya awali hadi vyuoni.

Kwa wale wanaopinga hilo, wamekuwa wakidai kuwa kinachowabeba Wakenya dhidi ya raia wa nchi nyingine za Afrika Mashariki, ni uwezo wao mkubwa wa kuzungumza Kiingereza na si uelewa wa mambo kulingana na elimu yao.

Uwezo mkubwa wa Wakenya katika kuzungumza Kingereza, umetokana na mfumo wao wa elimu ambapo kuanzia ngazi ya awali, masomo hufundishwa kwa lugha hiyo, hali inayomfanya mtoto anapofikia umri wa kuanza shule ya msingi, kuwa fundi wa kuzungumza Kingereza.

Lakini pia, wapo wanaodai kuwa Wakenya si kwamba ni watu walioelimika zaidi ya wengine ndani ya ukanda huu, bali kinachowabeba ni ujanja wao wa kuchangamkia fursa mbalimbali, lakini pia ‘ushapu’ wao unaobebwa na uchapakazi wawapo sehemu ya kazi.

Hali hiyo imeelezwa kuwa tofauti na ilivyo kwa Watanzania ambao wengi wamedaiwa kuwa wavivu, wakitumia muda mwingi kupiga domo sehemu za kazi na kuendekeza zaidi starehe bila sababu zozote za msingi.

Hebu tuone mfumo mzima wa elimu nchini humo unaoelezewa kuwabeba Wakenya na kuonekana kuwa wataalam zaidi ya wakaazi wengi wa nchi nyingine za Afrika Mashariki na Kati kwa ujumla.

Kwa ujumla, elimu nchini Kenya imekuwa ikizingatia mfumo wa 8-4-4 tangu mwishoni mwa miaka wa 1980, ikiwa ni miaka minane ya elimu ya msingi, ikifuatiwa na miaka minne ya shule ya upili, kisha miaka minne ya taasisi au chuo kikuu.

Mbali na hayo, pia kuna sekta kubwa ya shule za kibinafsi ambazo hushughulikia watu wa viwango vya maisha ya kati na ya juu, ambao kwa ujumla hufuata mfumo wa elimu ya Uingereza wa elimu ya sekondari na msingi.

Kati ya watoto wote nchini Kenya, asilimia 85 huhudhuria shule za msingi, asilimia 24 huhudhuria shule za upili na asilimia mbili hujiunga na taasisi za elimu ya juu.

 

Elimu ya Msingi

 

Kuna aina tatu ya shule za msingi: Shule za kutwa ambazo zinajumuisha shule nyingi za msingi; shule za bweni ambazo zimegawanywa katika vitengo vitatu, vile vya gharama ya chini, wastani na za gharama ya juu; na shule za maeneo kame.

Elimu ya msingi katika shule za msingi za serikali ilifanywa kuwa ya bure na ya kila mmoja (si ya lazima) Januari mwaka 2003.

Mfumo wa Harambee (yaani kuungana pamoja) huchangia pakubwa katika utoaji wa elimu ya shule za msingi nchini humo. Mfumo wa Harambee hugharamia takriban asilimia 75 ya shule za msingi nchini Kenya. Mtihani wa kitaifa wa shule za msingi nchini Kenya hufanywa mwishoni mwa masomo ya msingi.

Kimani Maruge, ambaye ni Mkenya, ndiye aliyekuwa mtu mkongwe zaidi ulimwanguni kujiunga na shule ya msingi. Ni mkulima ambaye hakuwa amesoma, alijisajili akiwa na miaka 84 baada ya kufahamu kuwa masomo ya msingi yalikuwa ya bure ambapo alifariki mwaka wa 2009 akiwa na umri wa miaka 89

Elimu ya Shule za Upili

Wanafunzi nchini Kenya katika shule za sekondari huchukua miaka minne kujiandaa kwa masomo ya taasisi. Wanafunzi wengi huanza kuyajenga maisha yao ya usoni kwa kujiendeleza katika masomo yatakayowapa kazi.

Mtihani wa kitaifa wa kadato cha nne hufanywa mwishoni mwa masomo ya shule ya upili. Mwaka 2008, serikali ilianzisha mpango wa kutoa elimu bure kwa shule za upili.

Kuna vitengo vitatu vya shule za sekondari: Shule za kibinafsi, shule zinazofadhiliwa na serikali na shule za harambee. Shule zinazofadhiliwa na serikali zina ushindani mkali unaosababisha mmoja kati ya watoto wanne kukubaliwa kujiunga nazo.

Kujiunga na shule ya upili hutegemea alama za mwanafunzi katika mtihani wake wa darasa la nane (K.C.P.E) na kwamba shule nyingi zinazofadhiliwa na serikali ni za bweni.

Shule za Harambee hazina ushindani mkali na zinajumuisha asilimia 75 ya shule zote za upili nchini ambapo wanafunzi wanaopata alama za chini katika mtihani wao wa darasa la nane hujiunga na shule za harambee, shule za kibiashara au kuacha shule.

Vifaa katika shule hizo si vizuri kama vile vya shule zinazo fadhiliwa na serikali na mara nyingi hukosa vitabu, walimu waliohitimu, madawati na mengineyo.

Shule nyingi za kibinafsi huwa na mfumo wa elimu ya Uingereza , ukifuatiwa na elimu ya sekondari ya juu (A-level) ya kimataifa licha tu ya chache zinazofuata mfumo wa Marekani. Shule chache za kibinafsi hufuata mfumo wa KCSE kando na mifumo ya kigeni wakiwapa wanafunzi kuchagua ni upi wa kufuatwa.

 

Taasisi za elimu

Hizi ni taasisi zinazotoa elimu ya juu kwa miaka miwili au mitatu katika viwango vya cheti, diploma na diploma ya juu ya kitaifa ambapo taasisi hizo hutoa mafunzo ya kiufundi kwa kutumia ujuzi wa mikono katika nyanja mbalimbali kama vile uhandisi sayansi ya madawa, elimu, sayansi ya kompyuta na mengineyo.

Zinajumuisha vyuo vya mafunzo ya ualimu (TTCs), taasisi za mafunzo ya udaktari nchini Kenya (KMTC), Kenya Polytechnic, Mombasa Polytechnic, Eldoret Polytechnic, Tasisi ya mafunzo ya utangazaji na nyingine nyingi ambapo taasisi hizo zote huanzishwa na miswada mbalimbali ya Bunge.

Vyuo vya umma

Vyuo vikongwe zaidi nchini Kenya ni pamoja na Chuo kikuu cha Jomo Kenyatta cha Kilimo na Teknolojia, Chuo kikuu cha Egerton, Moi, Chuo kikuu cha Mseno na Chuo Kikuu cha Masinde Muliro cha Sayansi na Teknolojia (zamani Chuo cha Mgharibi).

Usikose toleo la Mtanzania Ijumaa ijayo kufahanmu zaidi juu ya mfumo wa elimu Kenya, zaidi ikiwa ni jinsi sera ya Elimu Bure inavyoitesa nchi hiyo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles