23.3 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

WANAFUNZI 500 WATUMIA MATUNDU MAWILI YA CHOO

Na FLORENCE SANAWA-MTWARA

ZAIDI ya wanafunzi 513 wa Shule ya Msingi Mbae iliyopo Manispaa  ya Mtwara Mikindani, wanatumia matundu mawili ya choo.

Akizungumza na MTANZANIA shuleni hapo  wakati wa kuweka jiwe la msingi kwenye majengo ya vyoo vipya 10, Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo, Josephat Mussa, alisema tatizo hilo linaweza kuwasababisha uwepo wa magonjwa ya milipuko kwa wanafunzi hao.

Ujenzi wa vyoo hivyo unafadhiliwa na Shirika la Woman for Vision la mjini hapa.

“Shule yetu ilianza mwaka 2015 na ina darasa la awali, darasa la kwanza, la pili na la tatu na hadi sasa tuna madarasa matatu.

“Pamoja na kwamba wanafunzi wanasomea katika mazingira magumu, walimu nao wamekuwa wakifanya kazi katika mazingira ya aina hiyo kwa sababu hatuna ofisi na badala yake tunakaa chini ya miti katika kipindi chote tunachokuwa shuleni hapa.

“Yaani, hata hapa nilipo chini ya mti ndipo ilipo ofisi ya mwalimu mkuu na wakati huu wa msimu wa korosho, usishangae kuona korosho zinanidondokea.

“Kibaya zaidi, wakati mwingine unapokuwa kwenye maandalizi ya kipindi, nyoka anadondoka chini, yaani tuko katika hatari ya hali ya juu.

“Pamoja na shida hizo, sasa tumeona madiwani na mkurugenzi wa halmashauri, wamejitahidi kwa kiasi kikubwa tumepata matundu 10 mapya ya choo na pia tumepata ufadhili mwingine wametujengea mengine 10, lakini hatuna ofisi na tuna upungufu wa madarasa manane,” alisema Mussa.

Naye Mwenyekiti wa Shirika la Woman for Vision, Adelina Kalumuna, alisema kutokana na uhitaji mkubwa wa matundu ya vyoo katika shule nyingi katika manispaa hiyo, wamelazimika kuanza ujenzi wa matundu 20 ya vyoo katika Shule ya Msingi Mbae na Shule ya Msingi Maendeleo ambazo zilionekana kuwa na uhitaji mkubwa.

Akiweka jiwe la msingi  katika vyoo vya shule hizo, Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, Evod Mmanda, alisema shule hizo ni moja ya shule zenye changamoto nyingi za miundombinu ikiwamo vyoo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles