31.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Wanachama 15 NMB Business Club wapaa Uturuki

Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital

WAFANYABIASHARA 15 Wanachama wa Klabu za Biashara za Benki ya NMB (NMB Business Club), wameagwa jijini Dar es Salaam jana asubuhi na kuondoka jioni kwenda Istanbul, Uturuki kwa aziara ya siku tisa – kutembelea Maonesho ya Biashara ya Kimataifa (Trade Fairs 2022).
 
Hafla ya kuwaaga wafanyabiashara hao imefanyika Makao Makuu ya NMB, ambako Afisa Mkuu wa Mikopo wa Benki ya NMB, Daniel Mbotto, aliwakabidhi tiketi za safari hiyo, akishuhudiwa na Afisa Mkuu wa Huduma Shirikishi NMB, Nenyuata Menjooli na Mkuu wa Idara ya Biashara wa benki hiyo, Alex Mgeni.
 
Hii ni mara ya pili kwa NMB kuratibu ziara za aina hiyo, mara ya kwanza ilikuwa mwaka 2019, ambako wafanyabiasahara 10 walitembelea na kushiriki Maonesho ya 125 ya Canton Fair 2019, yaliyofanyika mjini Guangzhou, China, kabla ya janga la corona kukwamisha safari hizo miaka miwili ya 2020 na 2021.
 
Akizungumza kabla ya kuwakabidhi tiketi za safari zao kwenda na kurudi katika ziara hiyo iliyogharamiwa kila kitu na NMB, Mboto alisema lengo la kusafarisha wafanyabiashara hao ni kuwapa fursa ya kujifunza masuala mbalimbali muhimu kwa ustawi wa biashara zao.
 
Mbotto alibainisha kuwa, wafanyabiashara hao watawasili Uturuki saa 12 jioni ya Oktoba 18, kabla ya Oktoba 19, kuanza ziara ya kutembelea maonesho hayo ili kuwapa mwanga kibiashara na watakuwa huko siku 9 wakijifunza mengi kutoka kwa wafanyabiashara wa taifa hilo kubwa linaloendelea kwa kasi kibiashara
 
“Miongoni mwa maeneo watakayotembelea ni pamoja na viwanda vinavyozalisha bidhaa zenye soko kubwa nchini, ambazo wana uhusiano nazo, ambako watajionea uzalishaji wa bidhaa mbalimbali zikiwemo vifaa tiba, vifaa vya ujenzi, nguo, vipodozi na kadhalika.
 
“NMB tunaamini ziara yao hiyo 9 itakuwa na manufaa makubwa kwa wafanyabiashara hawa na taifa kwa ujumla wake, kwa kuwa kukua kwao kibiashara ni kuongezeka kwa ajira na manufaa kwa Watanzania wote,” alisisitiza Mbotto
 
Alivitaja vigezo vilivyotumika kupata wafanyabiashara hao kuwa ni pamoja na historia yao nzuri ya ukopaji na urejeshaji mikopo, kupitisha biashara zao kwa asilimia 95 katika benki ya NMB, kusaidia kwao kuunganisha wafanyabiashara kujiunga NMB na uwezo wa kuchangia asilimia kidogo za safari.
 
Mbotto aliwataka wafanyabiashara hao kuhakikisha ziara hiyo inalete mabadiliko yao kibiashara, wanatumia vema kila fursa watakayoiona na kurejea nyumbani wakiwa na ujuzi mkubwa, sambamba na kutanua mtandao wa kibiashara ili kukuza biashara zao na uchumi wa taifa.
 
“Niwakumbushe zaidi wafanyabiashara, kuna fursa nyingi ndani ya benki ya NMB na msisite kutuchagua sisi katika kufanya biashara zenu kwa tija na manufaa, ambako mbali ya huduma bora, tunazo nafasi adhimu kama hizi za ziara za kibiashara ambazo ni chachu ya ukuaji wao kiuchumi,” alisisitiza.
 
Naye mwakilishi wa wafanyabiashara 15 walio katika msafara huo, Paulo Lema, aliishukuru NMB kwa fursa mbalimbali inazotoa kwa wateja wao wa kada mbalimbali katika kuwaongezea nguvu ya kukua kiuchumi na kusisitiza kuwa kadri wanavyoshikwa mkono, wanarahisishiwa ukuaji wao kibiashara.
 
“Kadri NMB mnavyosapoti biashara zetu kwa kutupa mikopo, elimu ya fedha na fursa kama hizi, ndivyo mnavyoharakisha maendeleo na ustawi wetu kibiashara, tunawahakikishia Watanzania kwamba tutarejea tukiwa bora zaidi kutokana na matunda ya ziara hii. 

“Nia ni kukuza uwezo wetu katika kutoa ajira kwa Watanzania wenzetu kupitia fursa kama hizi, ambazo tunatoa wito pia kwa NMB kuendelea kutujali na kuwafikia wateja, wajasiriamali na wafanyabiashara zaidi ili kuwaongezea uelewa wa masuala ya kibiashara na kiuchumi,” alisisitiza Lema.
 
Akizungumza kwa niaba ya wafanyabiashara waliopata fursa kama hiyo mwaka 2019, Award Mpandila, ambaye ni Mwenyekiti wa NMB Business Club Mkoa wa Dar es Salaam, alikiri kuwa ziara yao katika Maonesho ya Canton Fair yamewasaidia kuwabadili kimfumo, kiuendeshaji na ufanyaji biashara.
 
“Ni ziara ambayo ilitupa faida mbalimbali, ambazo zimekuwa chachu za ukuaji wetu kibiashara kitaifa na kimataifa na kwa sasa tumefikia levo za kusaini mikataba mbalimbali wenzetu kutoka mataifa yaliyoendelea na hivyo kusapoti Tanzania ya Viwanda inayochakatwa na Serikali.
 
“Uwezeshaji tunaoendelea kuupata kutoka NMB ni mkubwa na wenye tija kwa biashara zetu, kampuni zetu, taasisi na mashirika yetu. Wito wangu kwenu mliopata fursa hii mwaka huu, tambueni mnawawakilisha maelfu ya wafanyabiashara na hivyo mkawe mabalozi wema wa benki huko Uturuki,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles