21.5 C
Dar es Salaam
Saturday, July 27, 2024

Contact us: [email protected]

Wamshukuru Mbunge Toufiq kwa mitungi ya Gesi ya Oryxy

Na Ramadhan Hassan, Chamwino

WAJASIAMALI waliopatiwa mitungi ya gesi aina ya Oryxy na Mbunge wa Viti Maalum, Fatma Toufiq (CCM) wameahidi kuachana na matumizi ya kuni na kujikita katika matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Juni 6,2024 Mbunge huyo alikabidhi mitungi 200 yenye thamani ya zaidi ya Sh milioni 9 kwa wajasiriamali na viongozi wa Jumuiya ya Wanawake wa Chama cha Mapinduzi (UWT) Wilayani Chamwino.

Wakizungumza mara baada ya kukabidhiwa mitungi hiyo,wajasiriamali hao walimshukuru Mbunge huyo huku wakiahidi kutorudia kutumia kuni.

“Asante Mheshimiwa Mbunge wewe ni wa kwetu unatusaidia kwenye mambo ya msingi ambayo yamekuwa msaada mkubwa kwetu pia tunamshukuru Mama Samia (Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania) kwa kuleta agenda ya nishati safi ya kupikia,” amesema Irene Jackson mjasiriamali katika katika kata ya Mbande.

Naye, Rehema Matonya, kutoka Kata ya Buigiri amesema mitungi hiyo itawasaidia kutunza mazingira na kuacha kutembea umbali mrefu kutafuta kuni hivyo kutumia muda mrefu kutunza familia.

“Tunamshukuru Mbunge na kampuni ya Oryx kwa kutupa mitungi hii hakika hii ni zaidi ya zawadi kwani tulikuwa tunapata changamoto ikiwemo kupata magonjwa kama TB,” amesema Matonya.

Kwa upande wake, Mbunge Toufiq amesema anamini mitungi hiyo itaendelea kulinda ndoa kwani kina mama watatumia muda mchache kupika chakula na kutotembea umbali mrefu.

“Tunaendelea kumuunga mkono Rais Samia katika matumizi ya nishati safi Mimi kama Mbunge wenu nitaendelea kupiga hodi katika maeneo mbalimbali ili lengo la asilimia 80 kutumia nishati analotaka Mheshimiwa Rais liweze kufikia,” amesema Mbunge huyo.

Amesema anaamini Wanawake wa Chamwino na Tanzania watahakikisha wanampigia kura Rais Samia ili aweze kuongoza kwa miaka mitano mingine.

Kwa upande wake, Meneja Mauzo Kanda ya kati kampuni ya Oryx, Jeniffer Mosha, amesema wanaunga mkono jitihada za serikali katika suala la utunzaji wa mazingira ambapo kwa Mkoa wa Dodoma watatoa zaidi ya mitungi 1,000.

Amesema anaamini kupitia mitungi hiyo wananchi watatunza mazingira huku akishauri kuitunza ili waweze kutumia kwa muda mrefu.

Katika hatua nyingine Mbunge Toufiq ameonesha kushangazwa na baadhi ya watu wanaojipitisha katika Jimbo la Chamwino na kuanza kampeni wakati muda bado haujafika.

Akizungumza katika kikao cha Baraza la Umoja wa Wanawake wa Chama cha Mapinduzi (UWT) Wilayani Chamwino Mbunge huyo amesema anajua baadhi ya viongozi wakubwa wamekuwa wakipita katika Jimbo hilo na kutoa lugha za matusi na kwamba yeye hafai.

“Kuna watu wanatembea na agenda ya ukabila na udini tena ni viongozi wakubwa wanaleta chuki,tunataka kuwaambia wawe na subira muda bado,Mungu anapanga amtakae,”amesema Mbunge huyo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles