27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Walimu Kenya kurudi kazini leo

sossion-strikeNAIROBI, KENYA

VYAMA vya walimu nchini vimetii agizo la mahakama, na hivyo kutangaza kusitisha mgomo na kuwaomba walimu kuripoti kazini kuanzia leo.

Katibu Mkuu wa Chama cha Taifa cha Walimu (KNUT), Wilson Sossion aliwataka walimu wote waliokuwa kwenye mgomo kurudi darasani akisema kuwa leo ni mwanzo mpya wa muhula wa tatu.

Aidha Chama cha Walimu wa Taasisi za Kati (KUPPET) pia kiliwaomba wanachama wake kurejea kazini.

Hata hivyo, Sossion alisema bado wana hofu kuwa serikali inalenga kuwasumbua walimu kwa kutoheshimu agizo la mahakama la kuwaongezea mishahara yao pamoja na kutowalipa ile ya mwezi Septemba.

“Walimu bado hawajapokea mishahara yao ya Septemba, hali inayotutia wasiwasi kuwa huenda hii ikawa ni njama ya kutusumbua zaidi,” alisema, alipowahutubia wanahabari katika Makao Makuu ya KNUT mjini hapa.

Sossion alikumbushia mishahara hiyo ni haki yao ambapo Tume ya Kuwaajiri Walimu (TSC) inapaswa kutekeleza agizo la kuwalipa.

Mkuu huyo pia alilitaka Baraza la Mitihani la Taifa (KNEC) kubadilisha tarehe za mitihani ili kuwapa walimu na wanafunzi muda wa kutosha ili kujitayarisha kwa mitihani ya taifa.

“Tungependa kuiomba KNEC kubadili ratiba ya mitihani ya taifa ili kutuwezesha kuwatayarisha wanafunzi ipasavyo,”

Sossion pia alilihakikishia baraza hilo kuwa KNUT ilikuwa imewaruhusu wanachama wake kusimamia mitihani hiyo kinyume na hapo awali ilipowakataza kushiriki katika usimamizi huo.

Mbali ya hayo, aliwaonya walimu wanaolengwa kuajiriwa na TSC ili kuziba pengo la waliogoma “kutokubali kutumiwa” bali kusimamia haki zao.

TSC ilikuwa imetangaza nafasi mpya za walimu 70,000 iliolenga kuwaajiri kwa njia ya kandarasi kwa miezi mitatu. Hata hivyo, hatua hiyo ilisitishwa na mahakama.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles