30.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

WAKATI SAHIHI WA KUWAANGALIA WAHITAJI

man-giving-poor-chid-shoes

Na ATHUMANI MOHAMED

LEO ni Disemba 3, ikiwa zimesalia takribani wiki tatu ili kufikia Sikukuu ya Krismasi na wiki nne kufikia Mwaka Mpya. Ni wakati wa sikukuu za mwisho wa mwaka ambapo wengi huwa kwenye mapumziko.

Hiki ni kipindi ambacho hata aina ya vyakula hubadilika kwenye nyumba nyingi. Kwa kawaida, katika jamii yetu, chakula kikuu huwa ni pilau – wali na nyama.

Ukipita mitaani katika siku za sikukuu, pua yako itaburudishwa na harufu nzuri ya vyakula hivyo. Lakini umewahi kujiuliza kuhusu wahitaji?

Je,unajua kuwa kwenye jamii yetu, wapo watu ambao kwa namna moja ama nyingine wanashindwa kumudu baadhi ya mambo muhimu kama mahitaji yao muhimu nk?

Tambua kwamba kuna hilo. Wapo watu wapo mstari wa mbele kuwasaidia watu wa namna hiyo. Wengine wameweka utaratibu wa kuwasaidia kila siku, kila wiki, kila mwezi na wachache kila mwaka.

Ukweli ni kwamba, siyo rahisi watu wote wenye mahitaji wakasaidiwa na watu wachache wanaofanya hivyo.

Muhimu kwako kufahamu ni kwamba, kusaidia kunaongeza baraka katika maisha yako na kipato chako. Kumsaidia mwenye uhitaji wa kweli, unafungua milango yako ya mafanikio.

Hakuna baraka yoyote, wewe kufurahia sherehe wakati wapo wengine wakihuzunika, wakiwa hawana hata uhakika wa mlo wa siku hiyo achilia mbali mavazi nk.

Kumpa furaha mwenye uhitaji kutaziachilia baraka zako na utajiongezea nafasi kubwa ya mafanikio kwenye maisha yako.

FAMILIA

Je, umejipangaje kwa ajili ya familia yako? Kama huna familia hiyo ni shauri nyingine, lakini ikiwa umeoa /umeolewa, lazima wewe na mwenzako mpange namna bora ya kufurahia sikukuu na watoto wenu.

Wanunulie watoto wenu nguo, tayarisheni vyakula na vinywaji vya kutosha mapema. Epuka matumizi ya zimamoto.

Mahitaji mengi katika nyakati za sikukuu, hupanda bei. Epukeni hilo kwa kununua mahitaji yenu mapema.

Wafurahishe watoto wako kwa kuhakikisha nao wanapata mavazi mapya kama watoto wengine. Katika hili ni vizuri kuangalia pia bajeti za wageni waliopanga kuja kuwatembelea na wale wa dharura.

Sikukuu ni wakati wa kutembeleana,lazima ujiandae na hilo mapema. Ni aibu kupata wageni ndipo uanze kufikiria mahitaji na wakati kuanza kukopa.

Zuia huzuni nyakati za furaha kwa kujipanga mapema. Kupata wageni ukiwa huna kitu ni kero na huenda ikakufanya ukajisikia vibaya kumbe ulikuwana nafasi kujipanga mapema.

NDUGU

Ndugu zako ni muhimu kuwaangalia. Angalia zaidi watu wazima na watoto. Mfano wazazi wako na ndugu wengine kwenye familia/ukoo.

Wazazi bila kujali hali zao kifedha, ni fahari kwao ikiwa utawaandalia zawadi. Kuwazawadia wazazi kipindi cha sikukuu si tu kwamba utawafurahisha lakini utawafanya wajivunie kuwa na mtoto kama wewe huku ukiwa na uhakika wa kuvuna baraka kutoka kwao.

WASIO NA UWEZO

Hili nimeshagusia kidogo wakati naanza kuandika makala haya. Ukweli ni kwamba kuwasaidia wanaohitaji,unajiweka kweye baraka kubwa.

Angalia nafasi yako kifedha, lakini unaweza kuwatazama zaidi wale unaoishi nao mtaa mmoja. Lazima utakuwa unajua familia zenye hali ya chini zaidi.

Wanunulie hata kilo kadhaa za mchele uwapatie. Malathani kama una uwezo wa kilo 50,unaweza kuzigawa kilo tano kwa familia 10 na ukawapatia wiki moja kabla ya wiki ya sherehe.

Kwa hakika utawarejeshea furaha yao, dua yao kwa Mungu wakishukuru muujiza wa kupata chakula utakuwa baraka katika mafanikio ya maisha yako. Wenye kujua siri hii, wana mafanikio makubwa maishani mwao.

Ni kanuni kubwa yenye matokeo ya haraka ambayo pia hutumiwa hata na mataifa makubwa kwa kusaidia mataifa yasiyo na maendeleo makubwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles