21.5 C
Dar es Salaam
Saturday, July 27, 2024

Contact us: [email protected]

Wakandarasi 7 wa Barabara Simiyu matatani

Na Derick Milton, Simiyu

Bodi ya Barabara Mkoa wa Simiyu imeagiza kufutiwa zabuni zilizotolewa kwa kampuni saba za Ukandarasi wa usafi wa barabara za lami mkoani humo kwa kosa la kutohudhuria vikao vya bodi hiyo mara mbili mfulululizo.

Bodi hiyo imesema kuwa Kampuni hizo licha ya kupewa taarifa kila kikao, wamekaidi kuhudhuria na hawajatoa taarifa za kwanini wao wameshindwa kufika kwenye vikao hivyo muhimu na vya kisheria.

Mbunge wa Maswa Mashariki, Stanslaus Nyongo, akizungumza wakati wa kikao cha Bodi ya Barabara Mkoa wa Simiyu, kilichofanyika leo Desemba 28, 2021.

Agizo hilo limetolewa leo Jumanne Desemba 28, 2021 na Mwenyekiti wa Bodi ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa huo, David Kafulila, wakati wa kikao cha bodi kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano mjini Bariadi.

Kafulila amesema kuwa wakandarasi wa kampuni hizo wameonyesha dharau ya kutoshiriki vikao vya kisheria mara mbili, hivyo hawastahili kufanya kazi ndani ya mkoa na ameigiza wakala wa barabara kuwafutia zabuni na kutangaza upya zabuni kwa watu wengine.

Awali, wakizungumza kwenye kikao hicho wajumbe walisikitishwa na Wakala wa Barabara (TANROADS) kutoa zabuni za usafi wa barabara hizo kwa wakandarasi kutoka nje ya Simiyu wakati ndani ya mkoa huo kuna wakandarasi wengi wenye uwezo na sifa ya kufanya kazi hiyo.

“Wakandarasi wengi ambao wamepewa kazi hizi za usafi wa barabara wengi wanatoka mikoa ya Shinyanga, Mara na Mwanza, kwa Simiyu yupo mmoja, hili jambo siyo jema, TANRODS wabadilike, vikudi vya ndani ya mkoa viwezeshwe na hizi kazi wachukue wananchi wandani ya mkoa wetu,” amesema Njalu Silanga (Mbunge).

Wakati akifungua kikao hicho, Kafulila ametoa onyo la mwisho kwa wakandarasi wa Barabara mkoani humo ambao wamepewa kazi na TARURA pamoja na TANROADS kuhakikisha wanajenga miradi hiyo kwa kiwango.

Mbunge wa Itilima mkoani Simiyu, Njalu Silanga akizungumza wakati wa kikao cha Bodi ya Barabara Mkoa wa Simiyu.

Kafulila amesema kuwa miradi mingi ambayo wakandarasi wamekuwa wakijenga, imekuwa chini ya kiwango ambapo ameeleza, hatosita kuwachukulia hatua wakandarasi watakaojenga barabara za lami na molamu chini ya kiwango.

“Kama Mkuu wa Mkoa sitasita hata kidogo kuchukua hatua kali kwa mkandarasi ambaye atajenga mradi wabBarabara chini ya kiwango, miradi hii ambayo wamepewa kwa sasa ni kipimo tosha kwa sasa,” amesema Kafulila.

Akitoa taarifa ya hali ya barabara Kaimu Meneja wa TANROADS Mkoa, John Mkumbo, amesema kuwa kumekuwepo na changamoto kubwa ya wizi wa viakisi mwanga (Reflectors) ambavyo vimekuwa vikiwekwa pembezoni mwa barabara.

“Mpaka sasa kwa barabara ya Bariadi – Maswa jumla ya viakisi Mwanga 120, vimeibiwa na wametoa taarifa jeshi la polisi kwa ajili ya kufanyia uchunguzi na kuwabaini wale wote ambao wanahusika na wizi huo,” amesema Mkumbo.

Naye Meneja wa TARURA Mkoa, Mhandisi Gaston Gasana, amesema kwa mkoa wa Simiyu barabara nzuri ni asilimia ni kilometa 931 sawa na asilimia 22.3,na za wastani ni.kilometa 1720 asilimia 41.3 na mbaya ni kilometa 1512 asilimia 36.

Mhandisi Gasana ameongeza kuwa kwa mwaka wa fedha 2021/2022 TARURA imekwisha saini mikataba 39 kwa ajili ya matengenezo ya barabara zake ambapo zaidi ya kilometa 1,080.38 zitafanyiwa matengenezo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles