27.2 C
Dar es Salaam
Thursday, May 2, 2024

Contact us: [email protected]

Wabunge waahidi kupatikana kwa sheria bora ya habari

*Waahidi kuishauri Serikli kuwa na sheria zenye uhai wa muda mrefu

Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital

Baadhi ya wabunge nchini wameahidi kuwa watahakikisha kuwa tasnia ya habari inapata sheria bora hususan katika mchakato wa mabadiliko unaoendelea hivi sasa ambao uliwasilishwa bungeni Februari 10, mwaka huu.

Miongoni mwa wabunge hao ambao wameahidi upatikanaji wa sheria bora ya habari ni Mbunge wa Mlalo mkoani Tanga(CCM), Rashid Shangazi ambaye Tanga ameahidi kushirikiana na wadau wa habari kuhakikisha tasnia hiyo inakuwa na sheria bora.

Shangazi ametoa kauli hiyo wakati alipokutana na timu ya Wadau wa Haki ya Kupata Habari (CoRI), jijini Dodoma Aprili 24, mwaka huu.

Katika mazungumzo yake, Shangazi ambaye ni Mjumbe wa Kamati ya Katiba na Sheria, ameeleza ukakasi uliopo kwa baadhi ya vipengele vya sheria vilivyomo kwenye muswada wa sheria uliwasilishwa bungeni Februari 10, 2023.

Akigusia hoja ya Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania(TEF), Deodatus Balile, kuhusu kuwekwa ukomo wa chini wa kiwango cha adhabu, Shangazi amesema jambo hilo hata mahakimu linawapa tabu.

“Tuliwahi kukutana na mahakama ambapo mahakimu tuliwaeleza watuambie baadhi ya changamoto wanazozipata katika utendaji kazi wao. Moja ya changamoto walilyoeleza ni sheria kuwawekea ukomo wa chini wa adhabu, jambo hilo wanasema linawapa tabu sana,” amesema Shangazi.

Kauli ya mbunge huyo ilitanguliwa na ya Balile aliposema, siyo kila kosa la mwandishi linastahili kifungo kama ambavyo sheria inaelekeza.

Balile alisema awali sheria ilikuwa inaelekeza kifungo kisichopungua miaka mitano na baada ya vikao na Serikali, muswada uliowasilishwa bungeni umepunguza na kuweka miaka mitatu.

“Siyo kila kosa kwa mwanahabari linahitaji kifungo, makosa yanatofautiana, wakati mwingine kosa linaweza kuhitaji mtu kupewa adhabu ya mwezi mmoja ama kifungo cha nje. Hii inategemea na uzito wa kosa, lakini sheria ilivyowekwa, inamlazimisha jaji kutoa kifungo kisichopungua miaka mitatu hata kama kosa ni dogo linalohitaji onyo,” alisema Balile.

Upande wake Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya TEF, Neville Meena amemfafanualia mbunge huyo kuhusu dhana ya sheria inayompa mamlaka Waziri mwenye dhamana kuzuia machapisho kutoka nje na athari yake.

“Kwanza katika ulimwengu wa sasa machapisho yapo kwenye mitandao, kuweka sheria kuzuia machapisho kunalenga dhana ya kuonesha kukabiliana na uhuru wa habari. Waziri anaweza kuamua kukataa kuingizwa labda gazeti lolote mfano la Kenya ama nchi nyingine kwa sababu tu, halitaki kutokana na mambo yake binafsi,” amesema Meena.

Bunge Shangazi ameeleza kuwa kwa wakati uliopo ni vigumu kuzuia machapisho hivyo sheria hiyo kuwa ngumu katika utekelezaji wake.

Saumu Mwalimu kutoka Baraza la Habari Tanzania (MCT) alieleza kwamba,
Mbunge Shangazi amewaeleza kwamba, mchakato wa sheria ya habari umekuja wakati mzuri kutokana na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye, kuwa na utayari.

“Waziri Nape amefanya kazi sana mpaka kufikia hapo, naamini bado mnayo nafasi ya kukutana naye maana ni muelewa na ana utayari,” amesema Saumu.

Upande wake, Salome Makamba amesema asilimia 35 ya mapendekezo ya wadau wa habari ni machache,nakwamba walau yangevuka asilimia 50 ama 60.

Amesisitiza kuwa kuna kila sababu ya kuishauri kamati kujumuisha mapendekezo yaliyoachwa kadiri itavyowezekana ingawa sio rahisi kubeba yote.

“Nimejifunza zaidi kutoka kwenu lakini kuna jambo tunapaswa kufanya ili kuwa na sheria bora. Asilimia 35 ya mapendekezo iliyoingizwa kwenye muswada ni ndogo, walau ingekuwa zaidi ya silimia 50 ama 60 ingawa sio rahisi kupita mapendekezo yote.

“Tutaishauri vizuri kamati pale tutapokutana ili kuangalia yale yaliyoachwa nje na umuhimu wa kuyajumuisha kwenye muswada,” amesema Salome.

Naye Mbunge wa Kilolo, Justin Ngamoga, akizungumza na Wakili James Marenga kutoka MISA TAN na Deus Kibamba ambaye ni mjumbe wa CoRI alisema, ni muhimu sana kuangalia marekebisho yake.

“Eneo la habari ni muhimu kwa jamii na nchi hivyo, inahitaji uangalizi wa kutunga sheria zitazowezesha uhuru ambao utaisaidia jamii na serikali. Sheria zake zinapaswa kutoa nafasi katika utendaji uliotukuka. Tutaangalia na kuishauri kamati namna bora ya kuwa na sheria zenye uhaii mrefu kwenye tasnia ya habari,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles