24.2 C
Dar es Salaam
Sunday, April 28, 2024

Contact us: [email protected]

Waandishi wa habari, azaki wapigwa msasa kilimo chenye tija

Na Clara Matimo, Mwanza

Waandishi wa habari nchini wamepewa mafunzo ya namna ya kuripoti habari za kilimo zenye tija huku asasi za kiraia zikitakiwa kushirikiana nao katika ufuatiliaji wa uwajibikaji jamii(SAM) na ufuatiliaji wa matumizi ya umma(PET) katika sekta ya kilimo ili ilete maendeleo kwa wananchi.

Baadhi ya washiriki wa warsha hiyo wakiwa katika mafunzo hayo.

Wito huo umetolewa jijini Mwanza Agosti 29, 2023 na mwezeshaji wa mafunzo hayo kutoka Shirika lisilo la serikali linalojishughulisha na masuala ya kilimo (ANSAF), Owen Nelson wakati akizungumza kwenye warsha ya kubadilishana uzoefu kwa kongani ya kilimo kati ya Azaki na waandishi wa habari kutoka mikoa ya Mwanza, Simiyu, Kagera, Singida, Shinyanga, Tabora na Kigoma.

Nelson amesema lengo la semina hiyo ni kuhamasisha vyombo vya habari na waandishi wa habari kushirikiana na Azaki kushiriki kwenye sekta ya kilimo.

“Lengo kubwa la dhana ya uwajibikaji  ni mtoa haki atoe haki na mpokea haki apokee haki anayostahili yaani uwajibikaji kwa watoa huduma na wapokea huduma, mfano Serikali ikitoa mbegu za zao fulani tunatarajia wapokea huduma ambao ni wakulima wazitumiea kama walivyoelekezwa na wataalamu wa kilimo ili kuwa na uwajibikaji tunawategemea sana waandishi wa habari.

 “Maisha bora kwa wakulima yatapatikana kama kutakuwa na kilimo bora chenye tija,  kama hakuna uadilifu hakuna uwajibikaji,” amesema Nelson.

Kwa mujibu wa Nelson warsha hiyo ya siku tatu iliyoanza Agosti 29 hadi 31, 2023 imekutanisha jumla ya washiriki 17, imeratibiwa na ANSAF kwa ufadhili wa The Foundation for Civil Society(FCS).

Nao baadhi ya washiriki wa warsha hiyo akiwemo, Paschal Michael, Mussa Masongo na Sudi Shaban wamesema wanatarajia kunufaika kupitia mafunzo watakayoyapata kwani yamewapa nafasi ya kujitathmini walipotoka, walipo na wanapotaka kwenda katika masuala mazima ya uwajibikaji katika rasilimali za taifa.

Mratibu wa Miradi kutoka Shirika lisilo la serikali linalojishughulisha na uchumi wa nyumbani(TAHEA), Mussa Masongo amesema mafunzo hayo ni msingi mzuri kwa kuwa yamewakutanisha pamoja wadau wa maendeleo kwani kwa pamoja wataisaidia jamii kuweza kuibua changamoto zinazowakabili katika sekta ya kilimo.

“Kama jamii itaelewa zana nzima ya uwajibikaji wa pamoja miradi mingi itaweza  kuwa endelevu na inayosimamiwa na jamii yenyewe maana jamii kubwa imekuwa na dhana   kwamba miradi inayotekelezwa na serikali ama wadau wa maendeleo haiwahusu hivyo kuwaachia wanaoitekeleza kuisimamia ama kuifuatilia.

“Lakini sasa kupitia warsha hii naamini endapo waandishi wa habari watatumia kalamu zao vizuri maana kalamu za waandishi ni jicho la wasioona ama sauti ya wasiosikika tukishirikiana nao sisi wadau wa maendeleo tunaweza tukafanya kazi kwa pamoja kwa sababu changamoto ni nyingi katika jamii yetu maana lengo ni kupata huduma bora,” amesema Masongo na kuongeza:

“Mafunzo haya yametufumbua macho maana kuna mambo mengine tulikuwa hatuyajui kwa mfano jinsi ya kufanya uchechemuzi kwa hiyo sisi kwetu wana azaki mafunzo haya ni bora na yamekuja kwa wakati,”ameeleza.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles