27.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

UVCCM yakemea ushoga, usagaji

Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital

Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Taifa, Mohamed Ali Kawaida amewataka vijana kuzingatia maadili ya Kitanzania na kuepuka kujihusisha na mapenzi ya jinsia moja ili kujenga kizazi bora kwa faida ya Taifa.

Mwenyekiti wa UVCCM Taifa, Mohamed Ali Kawaida, akizungumza wakati wa fainali za mashindano yaliyoandaliwa na Mbunge wa Segerea, Bonnah Kamoli.

Kawaida ameyasema hayo wakati wa fainali za mashindano ya soka na rede yaliyoandaliwa na Mbunge wa Jimbo la Segerea, Bonnah Kamoli na kufanyika katika uwanja wa Shule ya Msingi Tabata.

“Vijana lazima tuambizane ukweli, kuna tatizo kubwa la maadili na kwa bahati mbaya Dar es Salaam sasa hivi mnafuatia. Wewe umeitwa Juma baki kuitwa Juma, wewe uliyeitwa Fatuma hilo ndio jina lako linalokutosha…kuna ndugu zetu kina Mary na John mbaki na majina yenu.

“Haya mambo mengine waachieni wenyewe, Tanzania tuna mila na desturi zetu haya si mambo yetu,” amesema Kawaida.

Aidha amempongeza mbunge huyo kwa kufuata nyayo za Rais Samia Suluhu Hassan katika michezo na kuwataka Watanzania kuendelea kumtia moyo Rais Samia na kuliombea Taifa.

Kwa upande wake Bonnah amesema ameandaa mashindano hayo kwa lengo la kuibua vipaji vya vijana kwa sababu kupitia michezo wanaweza kupata fursa mbalimbali kama za ajira na kuimarisha afya zao.

Mashindano hayo yalianza kutimua vumbi Desemba 3 mwaka jana na kushirikisha timu 64 zikiwemo 61 za mitaa inayounda jimbo hilo, timu ya umoja wa bodaboda, timu ya umoja wa bajaji na timu ya UVCCM – Jimbo la Segerea.

Pia kulikuwa na timu 13 za mchezo wa rede ambapo kila kata imetoa timu moja.

Katika fainali hizo Bonyokwa walifanikiwa kutwaa kombe kwa mchezo wa soka na kuzawadiwa fedha taslimu Sh milioni 5 huku Kisiwani washindi wa pili wakizawadiwa Sh milioni 3 na washindi wa tatu Matumbi wakizawadiwa Sh milioni 2.

Kwa upande wa mchezo wa rede Buguruni waliibuka washindi na kuzawadiwa Sh 500,000 wakati washindi wa pili Mnyamani walizawadiwa Sh 300,000 na washindi wa tatu Kiwalani walizawadiwa Sh 200,000.

Aidha Mwenyekiti wa UVCCM pia aliwaongezea zawadi za fedha taslimu washindi wa mchezo wa rede ambapo Buguruni walipata Sh 500,000, Mnyamani Sh 300,000 na Kiwalani Sh 200,000. Pia alitoa Sh 200,000 kwa kila wilaya kwa ajili ya vikundi vya hamasa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles