Na Winfrida Mtoi, Mtanzania Digital
MABONDIA wa ngumi za kulipwa nchini, Cosmas Cheka na Muksin Swalehe, ‘Alkasusu’ wanatarajia kuzichapa Desemba 3, 2021 katika pambano lisilo la ubingwa lililopewa jina la Usiku wa Mshindo litakalopigwa kwenye Uwanja wa Kinesi, Dar es Salaam.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Novemba 18, jijini Dar es Salaam, promota wa pambano hilo ambaye ni Ofisa Habari wa Kampuni ya Grobox Sports Promotion waandaaji wa mchezo huo,Siah Mosha, amesema yatakuwepo mapambano mengine lakini Cheka na Alkasusu ndio litakuwa kubwa.
Amefafanua kuwa kampuni yao ni mpya na itajikita katika burudani mbalimbali, lakini wameamua kuanza na mchezo wa ngumi ili kuwakutanisha wababe hao na kumaliza ubishi.
“Tumezindua na kuitangaza kampuni yetu ya Grobox Sports Promotion ambayo itakuwa ikijihusisha na masuala ya burudani lakini kwa sasa tumeanza na mchezo wa ngumi ambao unakuwa kila kukicha,” amesema Siah.
Naye bondia Alkasusu amesema siku nyingi alikuwa anamtamani Cheka, imekuwa vizuri kwa promota huyo kuwakutanisha.
“Nimefurahi kukutanishwa na Cosmas Cheka, najua nitampiga na ninamuomba asikimbie kwa sababu ana tabia ya kusingizia kuumwa,” ametamba Alkasusu.
Kwa upande wake Cheka ameeleza kuwa yeye hana tabia ya kuongea sana mbivu na mbichi zitajulikana siku hiyo ulingoni.
“Tena niweke sawa mimi sina tabia ya kukimbia pambano. Kwanza Alikasusu anasema alikuwa anatamani kupigana na mimi siku nyingi ina maana kuna vitu amejifunza kwangu. Mimi ndiyo mhasibu wa ngumi napigana kwa mahesabu,” amejinadi Cheka.