25.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Ukusanyaji mapato wachochea mafanikio NSSF

*Ukuaji wake waimarika ikilinganishwa na miaka miwili nyuma

*Makusanyo yafikia Sh trilioni 4.3

Na Hadia Khamis, Mtanzania Digital

Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Masha Mshomba, amesema kuweka misingi imara na madhubuti ya ukusanyaji mapato kumechochea mfuko huo kukua kwa kasi ikilinganishwa na miaka ya nyuma.

Mshomba ameyasema hayo Dar es Salaam Agosti 19, 2022 wakati akitoa taarifa ya Utendaji wa Mfuko huo pamoja na vipaumbele vya Mfuko kwa mwaka wa Fedha 2022/23.

Mshomba amesema kuwa ukuaji wa mfuko huo ni mkubwa ikilinganishwa na miaka miwili iliyopita ambapo thamani ya mfuko ilikuwa ni Sh trilioni 4.3 nakwamba ukuaji huo umechochewa na ongezeko la makusanyo ya michango.

“Tumepata mafanikio makubwa katika suala zima la ukuaji wa mfuko na hii imesababishwa na sababu kadhaa ikiwemo kuweka misingi imara na madhubuti ya ukusanyaji wa mapato.

“Katika mwaka wa fedha 2021/2022 mfuko ulikusanya zaidi ya Sh trilioni 1.42 na makusanyo haya ni zaidi ya hata bajeti ambayo tulijipangia ambayo ilikuwa Sh trilioni 1.38,” amesema Mshomba.

Ameongeza kuwa mfuko huo umeboresha sana udhibiti wa matumizi jambo ambalo limechangia ukuaji wa NSSF.

Aidha, amebainisha mafanikio mengine kuwa ni uboreshaji wa huduma hasa kwa kutumia mifumo mbalimbali ya TEHAMA ambapo sasa mwanachama na wadau wanaweza kupata huduma popote walipo bila ya kufika katika ofisi za NSSF kwa kutumia mifumo ya waajiri na wanachama Employer Potal na Member Potal.

Mshomba amesema mfuko pia unapata matokeo mazuri katika uwekezaji hasa ukizingatiwa kuwa wanawekeza katika maeneo salama ambapo katika kipindi cha miaka miwili uwekezaji umeleta mapato makubwa.

“Ilikuwa haijafikia NSSF kupata mapato ya mwaka zaidi ya Sh bilioni 500 lakini katika mwaka huu wa fedha tumepata zaidi ya Sh bilioni 600.

“Matokeo haya ya uwekezaji yametokana na mfuko kujikita zaidi katika uwekezaji kwenye maeneo ambayo yanaleta faida kwa mfuko na kuhakikisha kunaudhibiti wa fedha,” amesema Mshomba.

Mshomba amesema chachu kubwa ya mafanikio ya NSSF imechagizwa na kasi ya utendaji wa Rais Samia Suluhu Hassan kwasababu ameongeza wawekezaji nchini hususan katika sekta binafsi.

“Tunamshukuru sana Mhe Rais Samia Suluhu Hassan amekuwa chachu ya mafanikio ya mfuko wetu kutokana na kufungua fursa za uwekezaji,” amesema.

Akizungumzia suala la waajiri kutowasilisha michango amesema wameweka mikakati mbalimbali kwa kushirikiana na taasisi nyingine za serikali ili kupata orodha kamili ya waajiri ambao watawafikia na kufuatilia michango ya wanachama.

Katika hatua nyingine Mshomba amewahamasisha Watanzania wote kushiriki katika zoezi la Sensa ya Watu na Makazi ifikapo Agosti 23, mwaka huu ili waweze kuhesabiwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles