24.8 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Ukata wakwamisha Tume ya Operesheni Tokomeza

Katibu Mkuu Kiongozi Ikulu, Balozi Ombeni Sefue
Katibu Mkuu Kiongozi Ikulu, Balozi Ombeni Sefue

NA MICHAEL SARUNGI

TUME iliyoundwa na Rais Jakaya Kikwete kwa ajili ya kuchunguza madhara yaliyotokea katika Operesheni Tokomeza Ujangili, hadi sasa inadaiwa haijaanza kazi kutokana na madai ya kutopatiwa fedha, MTANZANIA limebaini.

Uchunguzi uliofanywa na MTANZANIA, umebaini kuwa tume hiyo inayoongozwa na Mwenyekiti wake Jaji Mstaafu Hamisi Msumi haijaanza kazi .

Akizungumzia kutofanya kazi kwa tume hiyo, Katibu Mkuu Kiongozi Ikulu, Balozi Ombeni Sefue, alisema kazi ya ofisi yake ni kusimamia uteuzi na kama kuna jambo linalohusu utawala aulizwe Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

“Ofisi yangu ilishamaliza majukumu yake, majukumu yaliyobaki ni masuala ya kiutendaji, hebu muulize Mwanasheria Mkuu wa Serikali,” alisema Balozi Sefue.

Alisema yawezekana kuna matatizo madogo madogo ya kiutawala ambayo bado yanawatatiza, lakini kwa ufafanuzi wa kina hebu muulizeni Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

“Unajua ili tume hiyo ifanye kazi, wanahitaji vitu vingi vya kiutawala kama magari, ofisi na vitu vingingine vinavyohitaji maandalizi,” alisema Ombeni.

Alipotafutwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Federick Werema, alisema kuwa yeye si msemaji wa tume hiyo, na akamtaka mwanadishi kuwasiliana na Katibu Mkuu wa Tume, Frederick Manyanda ambaye hadi tunakwenda mitamboni hakupatikana.

Hata hivyo, alipotafutwa Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum, pamoja na manaibu wake wote hawakupatikana.

Tume hiyo iliyoteuliwa Mei 2, mwaka huu na kutangazwa na Balozi Sefue inaelezwa hadi sasa haijaanza kazi licha ya mwenyekiti na katibu wake kuapishwa na Rais Kikwete.

Novemba 18, mwaka jana Rais Kikwete alipokuwa akihutubia Bunge, aliahidi kuunda tume hiyo ili kufanya uchunguzi wa madai ya ukiukwaji wa haki za binadamu wakati wa Operesheni Tokomeza.

Rais Kikwete, alimteua Jaji mstaafu Hamisi Msumi kuwa mwenyekiti wa tume hiyo ya uchunguzi kuhusu vitendo vilivyotokana na uendeshaji wa operesheni hiyo.

Pia aliwateua Jaji Stephen Ihema na Jaji Vincent Kitubio Lyimo kuwa makamishna pamoja na Frederick Manyanda, Wakili wa Serikali katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuwa katibu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles