23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

TWENDE KIMATAIFA LAKINI TUSISAHAU NEMBO YETU

NI jambo la faraja kuona kwamba wakati tunaelekea ukingoni mwa mwaka huu wa 2017, kuna mafanikio makubwa kwenye  muziki wa Bongo Fleva. Juhudi kubwa inayofanywa na wasanii wetu inaridhisha na tumeona namna tunavyoweza kutembea kifua mbele.

Bongo Fleva ni muziki wenye heshima kubwa sasa. Tumeshuhudia namna ambavyo wasanii wetu wakizidi kuzoa tuzo mbalimbali za kimataifa kwa kufanya vizuri na kuwaacha wengine.

Kwa hakika ni mafanikio makubwa. Lakini tumeona mwaka huu katika tamasha kubwa la muziki la Fiesta ambalo mara nyingi kama siyo zote limekuwa likijumuisha na msanii mkubwa wa kimataifa, lakini mwaka huu Bongo Fleva walisimama wenyewe.

Jibu lilikuwa moja tu. Kuwadhihirishia wapenda burudani kuwa muziki wetu kwa sasa una hadhi ya kimataifa na unaweza kusimama wenyewe hata nyumbani. Ndivyo ilivyokuwa kwenye maonyesho hayo yaliyoanzia mikoani na baadaye kuhitimishwa pale kwenye Viwanja vya Leaders Club, jijini Dar es Salaam kwa shoo ya kufa mtu.

Tumeshuhudia namna wasanii wetu walivyoamka na kufanya mambo makubwa ya maendeleo huku wengine wakiwekeza kwenye biashara mbalimbali nje ya muziki wa Bongo Fleva.

Kwa wale ambao wamefanya vizuri kuupelekea muziki wetu nje ya mipaka yetu, Diamond anaweza kuwa mfano mzuri. Amefanya kolabo na wasanii wengi wa kimataifa mwaka huu wakiwemo Neyo, kundi la Morgan Heritage na Rick Ross.

Jambo la muhimu kwa Diamond na wasanii wengine wanaofanya kolabo na wasanii wa nje ni kutojisahau na kuingia kwenye mikito yao na kusahau ya kwetu. Ukiangalia nyimbo alizofanya Diamond na hao ni kama na yeye ni Mmarekani tu.

Juhudi zaidi zinatakiwa ili msanii wa Bongo anapofanya kolabo na wasanii wa nje, basi ijulikane kweli pale kuna mkono wa msanii wa Bongo Fleva na Mmarekani na siyo wao watufunike au tulazimishwe kuelekea kwenye mikito yao.

Bado tunayo kazi kubwa kuelekea huko lakini angalau basi tuna mwanzo mzuri wa kuwa karibu nao, kutambuliwa nao na kufanya nao kazi. Maana yake ni kwamba kama ni fursa tayari imeshafunguka, ni suala la kujipanga na kufanya kazi zaidi na zaidi ili kujitangaza.

Nawatia moyo wasanii wetu wa Bongo Fleva, kwa hakika mmefanya kazi nzuri kwa mwaka huu wa 2017 na bila shaka tutakapoingia mwaka 2018, tutakuwa na mafanikio makubwa zaidi ya kujivunia.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu wabariki wasani wetu nchini.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles