23.8 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Tume kuchunguza tuhuma dhidi ya Temesa Simiyu

Na Derick Milton, Simiyu

Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Miriam Mmbaga amesema kuwa ofisi yake itaunda tume kuchunguza madai ya madereva wa magari ya Serikali dhidi ya wakala wa ufundi na umeme (TEMESA) mkoani humo kutengeneza magari chini ya kiwango.

Mmbaga ametoa kauli hiyo leo Jumatatu, Januari 11, kwenye kikao cha madereva wa magari ya Serikali Mkoa mzima, polisi, TEMESA, ambacho kilikuwa na lengo la kujadili changamoto zinazowakabili kilichofanyika mjini Bariadi.

Mbali na hilo Mmbaga amesema tume hiyo itachunguza pia wizi wa vipuli vya magari uliopo kwenye taasisi hiyo, ambao ulilalamikiwa na madereva kufanywa na watumishi wa Temesa.

“Madereva wamesema hapa, Temesa mmnalipwa fedha za matengenezo lakini hamtengenezi, wakati mwingine mnaweka vipuri feki, vilivyotumika, Ofisi yangu itaunda tume kwa ajili ya kuchunguza haya yote.

Sehemu ya washiriki

“Hizi ni pesa za serikali lazima zitumike ipasavyo, tutaangalia pesa zilizolipwa na matengenezo yaliyofanyika ili tujue nani mchawi katika hili kama ni madereva, maafisa usafirishaji, au TEMESA,” amesema Mmbaga.

Katika kikao hicho madereva hao walilalamikia Temesa kwa wizi wa vipuri vya magari, lugha mbaya kwa baadhi ya wafanyakazi, kutokuwa na mapumziko kwa mafundi wa magari, kutotengeza ipasavyo magari licha ya kulipwa kiasi kikubwa cha fedha.

“Kama madereva tunaomba mkoa mtutafutie sehemu nyingine ya kupeleka magari yatengenezwe, hawa TEMESA hawana uwezo, ukipeleka magari kwao wanaharibu zaidi huku gharama zao zikiwa kubwa, wanaweka vipuri feki au chakavu wakati umelipa ili waweke vipya,” amesema Ramadhan Mohamed.

Kwa upande wake Kaimu Meneja TEMESA Mkoa wa Simiyu, Ardhiwani Jumanne amesema kuwa Taasisi hiyo inakabiliwa na changamoto kubwa ya kutokuwa na fedha za kutosha, hali ambayo imesababisha uwepo wa malalamiko hayo kutoka kwa madreva.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles