27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Trump atishia kurudisha nia ya kumshtaki Hillary

RAIS mteule Donald Trump wa Marekani na aliyekuwa mpinzani wake katika kinyang’anyiro cha urais, Hillary Clinton
RAIS mteule Donald Trump wa Marekani (kushoto) na aliyekuwa mpinzani wake katika kinyang’anyiro cha urais, Hillary Clinton.

WASHINGTON, MAREKANI

RAIS mteule Donald Trump wa Marekani, ametishia kufikiria upya ahadi aliyoitoa ya kutomfungulia mashtaka aliyekuwa mpinzani wake katika kinyang’anyiro cha urais, Hillary Clinton.

Trump ametoa tisho hilo kufuatia taarifa kuwa timu ya kampeni ya Hillary itashiriki kuhesabu kura upya katika Jimbo la Wisconsin, ambalo bilionea huyo alishinda.

Uamuzi wa timu hiyo unatokana na aliyekuwa mgombea urais kupitia Chama cha Kijani, Dk. Jill Stein, kuwasilisha hati ya kuhesabiwa upya kura katika jimbo hilo.

Hili ni pamoja na kuwa tangu mwanzo timu ya Hillary ilishasema haioni ishara zozote za kukiukwa sheria katika kinyang’anyiro hicho cha kuingia White House.

Msaidizi wa Trump, Kellyanne Conway, alisema iwapo timu ya Hillary itaendelea kushinikiza azma ya kutaka kushiriki kuhesabu kura upya, Trump hatasita kufikiria upya ahadi aliyoitoa ya kutomchukulia hatua kutokana na kutumia barua pepe binafsi wakati alipokuwa waziri wa mambo ya nje.

Aidha Trump alimkumbusha Hillary kuwa alishakubali matokeo na kabla ya uchaguzi pia aliahidi atakubali kushindwa.

Lakini wakili wa masuala ya uchaguzi wa Chama cha Democratic, Marc Erik, alisema harakati zao kuwezesha kuhesabu upya kura zitaendelea kufanyika hata katika majimbo mengine mawili ya Michigan na Pennsylvania.

Hata hivyo, wataalamu wa masuala ya uchaguzi walisema kutokana na matokeo ya jumla kuonyesha Hillary alikuwa nyuma ya Trump kwenye majimbo mengi, itakuwa ngumu kubatilisha ushindi.

Tisho la kambi ya Trump limeenda sambamba na bilionea huyo kudai kwamba watu milioni mbili walipiga kura kinyume cha sheria.

Alitoa kauli hiyo kufuatia Hillary kuongoza kwa pengo la kura za wananchi milioni 2, lakini ni Trump ameibuka mshindi kwa kupata kura nyingi za wajumbe kuliko mpinzani wake.

Trump pia alidai kulitokea ulaghai mwingi katika upigaji kura majimbo ya Virginia, New Hampshire na California ambako Hillary alishinda.

Na aliwashutumu wanahabari wa Marekani akisema wamekataa kuangazia suala hilo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles