
JOHANNESBURG, AFRIKA KUSINI
MAWAZIRI watatu katika Serikali ya Afrika Kusini, wamemtaka bosi wao, Rais Jacob Zuma ajiuzulu mwenyewe kabla hawajachukua hatua ya kumng’oa.
Tukio hilo lililoripotiwa jana na vyombo vya habari nchini hapa, linamweka Zuma katika wakati mgumu zaidi kisiasa tangu alipochukua madaraka mwaka 2009.
Shirika la Habari la News24 likinukuu duru ndani ya chama tawala cha African National Congress (ANC), lilisema tukio hilo lilitokea katika kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya chama hicho.
Katika kikao hicho, Waziri wa Utalii, Derek Hanekom, Waziri wa Afya, Mostsoaledi na Waziri wa Shughuli za Umma, Thulas Nxesi, walimtaka Zuma aondoke madarakani la sivyo NEC ipige kura kumng’oa.
Msimamo wao uliungwa mkono kwa nguvu na mnadhimu mkuu wa ANC, Â Jackson Mthembu.
Zuma anatuhumiwa uhusiano wake usiofaa na familia tajiri ya Kiasia ya Gupta, sambamba na kashfa ya ukarabati wa nyumba yake ya Nkandla ambazo zimeporomosha umaarufu wa ANC.
Mkutano huo wa NEC uliokuwa uishe juzi, lakini ukasogezwa hadi jana, ulishuhudia mgawanyiko na msuguano mkali kuhusu hatima ya Zuma.
Kwa mujibu wa vyanzo vya habari, wafuasi wa Zuma ndani ya kikao hicho wapatao 30 walipinga hoja iliyowasilishwa na Hanekom kutaka Zuma ajiuzulu.
Inasemekana wale wanaotaka kuondoka kwa Zuma wanapigania iwepo kura ya siri kuamua hatima ya rais.
Hilo linaonekana kuwapo mgawanyiko si katika chama hicho, bali pia Serikali ya Zuma na kuzua maswali namna gani ataweza kufanya kazi na wale wasio na imani naye.