23.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Tanzania na Korea zasaini mkataba wa Sh bilioni 684.6 kusukuma maendeleo

Na Ramadhan Hassan, Dodoma

Serikali ya Tanzania imesaini mkataba na Serikali ya Jamhuri ya Korea utakaoiwezesha serikali ya Tanzania kupata mikopo yenye masharti nafuu kutoka Mfuko wa Ushirikiano wa Kiuchumi wa Korea (EDCF) wenye thamani ya na Sh bilioni 684.6 kwa ajili ya kugharamia miradi mbalimbali.

Akizungumza wakati wa utiaji saini wa mkataba huo  leo, Desemba 8 mwaka huu, jijini Dodoma, Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Doto James ameitaja miradi itakayotekelezwa kuwa ni pamoja na Ujenzi wa Vituo viwili vya kupoozea Umeme katika njia ya kusafirisha umeme ya Kigoma – Nyakanazi (Grid ya Taifa ya Kaskazini Magharibi), wenye thamani  ya Sh bilioni 102.9. 

Pia, kusaidia bajeti kuu ya serikali, Sh bilioni 91.4 ili kuziba pengo la kibajeti lililotokana na madhara ya virusi vya corona.

Ameutaja mradi mwingine ni wa uboreshaji wa huduma za majitaka katika Jiji la Dodoma, wenye thamani ya Sh bilioni 160.

Katibu Mkuu huyo ameutaja mradi mwingine ni wa kuimarisha miundombinu ya upimaji na ramani,wenye thamani ya Sh bilioni 148.6.

Ameutaja mwingine ni wa ujenzi wa daraja jipya la Selander, wenye thamani ya Sh bilioni 74.5 ambao ni mkopo wa nyongeza. 

“Kwa niaba ya serikali ya Tanzania, napenda kukushukuru wewe binafsi na kupitia wewe EDCF, Serikali ya Jamhuri ya Korea kwa mchango huu muhimu ambao utaimarisha mahusiano yetu ya kirafiki yaliyodumu kwa miaka mingi kwa ajili ya uboreshaji wa maisha ya watu wetu,”amesema Katibu Mkuu. 

Katibu Mkuu huyo alimhakikishia Balozi wa Korea kuwa Serikali ya Tanzania itahakikisha kuwa fedha hizo zinatumika kama ilivyokusudiwa ili kufikia malengo ya miradi husika.

Kwa upande wake, Balozi wa Korea Nchini, Cho Tae Ick amesema kwamba nchi yake itaendelea kushirikiana na Tanzania kuendeleza miradi ya maendeleo kwa ajili ya uboreshaji wa maisha ya watanzania.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles