27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

SUMAYE ASEMA CCM IMEOTA ‘KUTU’

NA CHRISTINA GAULUHANGA -DAR ES SALAAM

WAZIRI Mkuu mstaafu, Fredrick Sumaye amesema Chama Cha Mapunduzi (CCM), kimekaa muda mrefu madarakani kimeota kutu hivyo kinastahili kuondolewa.

Sumaye ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema aliyasema hayo jana katika mkutano wa hadhara wa kumnadi mgombea ubunge wa Chadema, Salumu Mwalimu.

Alisema alichojifunza chama kikikaa muda mrefu madarakani kinaota kutu kichwani hivyo kuna kila sababu ya kukiondoa chama tawala madarakani ifikapo 2020.

“Kuna mambo yanashangaza mno tangu enzi za marais waliopita tulikuwa tunaangalia Bunge letu kupitia televisheni ya taifa lakini leo watu wachache wanazuia ili wananchi wasione uovu wa Serikali,”alisema Sumaye.

Alisema ili Kinondoni isonge mbele kuna kila sababu  ya kumchagua Mwalimu ambaye kwa vyovyote vile hata mwonekano wake haufanani na mgombea wa CCM.

Meya wa Manispaa ya Ubungo, Boniface Jacob aliwataka wana Kinondoni wasikubali kuuziwa mbuzi kwenye gunia.

Alisema kinachofanyika kwa sasa ndani ya CCM ni maagizo ambapo hata baadhi ya makada ndani ya chama hicho wameshangazwa na uteuzi wa Mtulia kuwa mgombea wao.

“Kinachowauma CCM ni baada ya Chadema kumsimamisha Mwalimu Kinondoni nami nipo viwanja vyangu vya kujidai nyumbani nilikozaliwa,”alisema.

Akizungumza katika mkutano huo, Mwalimu alisema anaifahamu vema Kinondoni hivyo hawezi kubabaishwa na wakuja.

Mwenyekiti wa Baraza la Vijana wa Chadema (Bavicha), Patrick Ole Sosopi alisema wamerudi kuomba nafasi ndani ya jimbo hilo kwa malengo.

“Naomba watambue hatujarudi katika jimbo hili kwa bahati mbaya kwa sababu mgombea wetu ni tofauti na Mtulia tunachoomba uchaguzi uwe huru na wa haki,” alisema Sosopi.

Alisema taswira inaonyesha uchaguzi wa marudio katika Jimbo la Kinondoni na Siha ni za kitaifa na zimekuja kwa sababu ya ubinafsi wa mtu mmoja.

Meneja wa kampeni wa Mwalimu, Said Kubenea alisema usaliti na madeni umesababisha Mtulia ahamie upande wa pili ili kuendelee kucheza na maisha.

Kubenea ambaye ni Mbunge wa Ubungo alisema Mtulia ana deni la mkopo wa Sh milioni 500 katika benki na mikopo mingine ya Sh milioni 90  na milioni 105 hivyo anadaiwa jumla ya Sh milioni 605.

“Mtulia amechezea maisha kwani anadaiwa Sh milioni 605 hana hata nyumba aliyojenga kwa sababu ya usaliti wake sasa anahaha,” alisema Kubenea.

Alisema katika kipindi cha bomoabomoa iliwalazimu wamchangie Sh milioni 20 ili awalipe mawakili waliokuwa wakimdai.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles