YOKOHAMA, JAPAN
KIUNGO mshambuliaji wa Manchester City, Raheem Sterling amesema alifurahi kuona klabu yake ya zamani ya Liverpool ikishinda taji la Ligi ya Mabingwa msimu uliopita.
Liverpool ilitwaa taji hilo, baada ya kuichapa Tottenham Spurs bao 1-0 katika mchezo wa fainali uliochezwa Uwanja wa Wanda Metropolitano Madrid, Hispania .
Hata hivyo, mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 24, alisema kuwa Manchester City kushinda taji la Ligi Kuu England ilikuwa muhimu zaidi.
Sterling aliondoka Merseyside mwaka 2015 na kujiunga na Man City katika hali ambayo iliwachefua mashabiki wa Liverpool kutokana na nyota huyo kulazimisha kuondoka katika kikosi chao, akiwa mchezaji muhimu.
“Nilifurahishwa sana na wao kushinda taji hilo, nimefurahi baadhi ya wachezaji ambao kuchukua ubingwa Ligi ya Mabingwa, ni jambo kubwa kwetu, lakini jambo letu muhimu zaidi ni kushinda Ligi Kuu hilo ndilo lengo letu kuu kuelekea msimu ujao.
“Ndiyo, itakuwa vizuri kushinda Ligi ya Mabingwa lakini kwanza tunataka kushinda ligi.Ligi Kuu ni mkate na siagi yako, kila wikiendi unajifunza kitu kipya , Ligi ya Mabingwa ndiyo inayoonekana vizuri na ya kifahari kama watu wanavyosema, lakini kila mwishoni mwa wiki unahama kwenda kukutana na mazingira magumu,”alisema Sterling.
City ilishinda taji la Ligi Kuu Eng;and katika dakika za mwisho msimu uliopita, ikimaliza msimu ikiwa na pointi 98, ikifuatiwa kwa karibu na Liverpool iliyomaliza na pointi 97.